Karibu!

Tunakukaribisha kwenye tovuti rasmi ya Msemaji Mkuu wa Serikali upate taarifa na habari sahihi zenye kuakisi malengo ya Serikali, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na matarajio ya Watanzania.

Mawasiliano

Tufuatilie

Na Adelina Johnbosco – MAELEZO Barabara za Mzunguko Jijini Dodoma imechangia kwa kiasi kikubwa kuondoa msongamano wa magari katikati ya jiji, hususan magari makubwa ya mizigo ya ndani na yanayokwenda nchi za nje. Mradi huu wa barabara ya njia nne kwa kiwango cha lami una urefu wa jumla ya kilometa 112.3 huku sehemu ya kwanza (lot 1) yenye kilometa 52.3 ikiwa imekamilika kwa asilimia 93.3. Barabara hii imeunganisha barabara kuu za mikoa minne, bandari kavu Ihumwa – Morogoro, Veyula – Arusha, Nala – Singida na Matumbulu – Iringa ambako sehemu ya pili ya ujenzi (lot 2) inaanzia. Shughuli za usafiri na usafirishaji tayari zimeanza katika barabra hiyo, watumiaji wanashuhudia urahisi wa safari kutokana na kutokuwepo foleni.  Imeturahisishia sana, inafanya safari iwe fupi kutokana na ukweli kwamba njia hii haina foleni hata kidogo kama kule mjini kati, mwanzoni kutoka Ihumwa hadi Nala ilikuwa tunatumia takribani saa na nusu hata zaidi, lakini kwa sasa tunatumia dakika 45 hadi 48 kwa safari hiyo hiyo” Bw. Simon Ndamanyilu, dereva lori Akitoa ufafanuzi kuhusu barabara hiyo hivi karibuni, Mhandisi Morice Mlay, kutoka kampuni ya mzawa ya  Inter-Consult Ltd (Mhandisi Mshauri wa Mradi), amesema barabara hiyo tayari imeanza kutumika na inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Oktoba, 2026 ambapo itakuwa imekamilika kabisa. “Ujenzi sehemu ya kwanza umefikia ukingoni, bado baadhi ya vitu vichache sana ikiwemo taa za barabarani na umaliziaji wa njia za watembea kwa miguu, magari mengi yanapita na yanapata urahisi kwa sababu hakuna foleni kwenye njia hii, mfano magari yanatoka moja kwa moja kutoka eneo la mzunguko wa Ihumwa hadi Nala ile barabara inayounganisha barabara ya Iringa bila kusimama popote” ametanabaisha Mha. Mlay Barabara hiyo ya njia nne yenye njia mbili kila upande, zimetenganishwa na uwazi katikati kwa ajili ya matumizi mengine pindi itakapohitajika kuongeza miundombinu mingine au uboreshaji. “Kuna baadhi ya watu wanashangaa kuhusu hili tuta lililoachwa katikati, hili ni kwa ajili ya matumizi ya baadaye mfano ujenzi wa barabara za mwendo kasi au kitu chochote kitakachoamuliwa kufanyika, lengo kuu ni kuepuka kutobomoa barabara kwa ajili ya kufanya kitu kipya” – Mha. Mlay  Baadhi ya wananchi jijini Dodoma wanaonesha furaha yao kutokana na uwepo wa barabara hiyo mpya inayopitisha magari mengi hasa magari makubwa ya mizingo kwenda ndani na nje ya nchi kwa wakati mmoja. Kwa mujibu wa Mha. Mlay, yapo magari yanayoelekea nchini Rwanda, Congo na Burundi kupitia barabara ya mzunguko. Katika eneo la Nala ambako kuna mojawapo ya makutano ya barabara hiyo na sehemu ya maegesho ya magari, wakazi wa maeneo hayo wamepata fursa ya kufanya biashara kutokana na uwepo wa watu wengi kwa wakati mmoja. “Kituo hiki yanapitisha na kusimama magari ya kila aina, hii ni tofauti na mwanzo, magari yakisimama hapa watu wanashuka na wengine wanakuwa wamesubiria kupanda, wengine ni madereva wa magari makubwa, kwa hiyo lazima watahitaji kupata mahitaji kutoka kwetu hasa chakula, hii ni furaha kwetu” Mary John, mama ntilie Tamanio la wengi ni kuona barabara inaanza kazi rasmi kwani kwao ni tegemeo mojawapo la njia ya kuongeza kipato. Kama kwa sasa nauza bidhaa zangu kwa kiwango ambacho naona kinafaa, nawaza kwamba barabara hii ikianza kutumika rasmi magari yataongezeka, yataegeshwa kwa wingi zaidi na watu watakuwa wengi kuliko hivi” amesema Bi. Veronica Alfred, muuza nafaka eneo la Nala. Mussa Rajab mkazi wa Nala na mkuli eneo hilo, akiwawakilisha wabeba mizigo wenzake, anasema uwepo wa sehemu ya kisasa ya kuegesha magari umefanya kazi yao kuwa rahisi na kukuza kipato. “Mwanzoni eneo hili halikuwepo, hivyo kusimama kwa magari hapa ilitegemea udharura wa dereva hapo na sisi tunavizia kubeba mizigo japo kwa uchache sana, siku hizi magari yanasimama na mizigo inateremshwa hivyo tunabeba na kupata riziki” – Bw. Rajab Mradi huu kipande cha kwanza utagharimu shilingi bil. 100.84 hadi kukamilika kwake, na unatarajiwa kuwa mwarobaini wa msongamano wa magari katikati ya jiji pia kukuza uchumi wa mkoa wa Dodoma, mikoa ya jirani na nchi kwa ujumla.

Na Timothy Mwakyenda – MAELEZO Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali amesema kuwa mafanikio ya Tamasha la Lugha ya Kiswahili lililofanyika nchini Ufaransa yamefungua ukurasa mpya wa kuitangaza lugha ya Kiswahili duniani na kuifanya kuwa nyenzo muhimu ya kukuza uchumi, biashara na diplomasia ya Tanzania. Akizungumza Julai 8, 2026, alipotembelea Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), Msigwa amesema kuwa ushiriki wa Tanzania katika tamasha hilo umeonyesha kuwa Kiswahili sasa si lugha ya mawasiliano pekee, bali ni rasilimali yenye uwezo wa kufungua fursa za kiuchumi kwa Watanzania.   Msigwa ameendelea kusema kuwa mataifa mengi yaliyofanikiwa kiuchumi yamenufaika pia kwa kutumia lugha zao kama chachu ya biashara na ubunifu, hivyo Watanzania wanapaswa kukitumia Kiswahili kama nyenzo ya kutangaza bidhaa, huduma na utamaduni wao katika soko la kimataifa. ” Baada ya mafanikio ya tamasha hilo, taasisi za Serikali na sekta binafsi zinapaswa kujipanga kimkakati ili kutumia fursa zinazotokana na kuongezeka kwa matumizi ya Kiswahili duniani, hatua itakayochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yenye lengo la kujenga uchumi wa dola za Marekani trilioni moja”, amesisitiza Msigwa. Akihusisha ujumbe huo na Maonesho ya Sabasaba, Msigwa amefafanua kuwa maonesho hayo yanatoa jukwaa muhimu la kuhamasisha uzalishaji wa bidhaa za ndani, ubunifu wa teknolojia na uongezaji thamani wa mazao, akitaja mfano wa vijana wa DIT ambao wametengeneza bajaji ya umeme na wafanyabiashara wanaochakata mazao kama korosho na parachichi na kusisitiza kuwa maendeleo hayo yanapaswa kuungwa mkono ili kuongeza ajira, kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje na kuhakikisha fedha nyingi zaidi zinabaki kuzunguka ndani ya uchumi wa Tanzania. Aidha, amewataka Watanzania kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi kwa kuelekeza nguvu katika uzalishaji, biashara, kilimo, viwanda na ubunifu badala ya kushawishiwa na ajenda zinazoweza kuvuruga maendeleo ya Taifa. Sambamba na hilo amewahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya Sabasaba ili kujifunza teknolojia mpya, kupata maarifa kutoka kwa washiriki wa ndani na nje ya nchi na kutumia fursa hizo kuboresha shughuli zao za kiuchumi huku akibainisha kuwa ongezeko la idadi ya nchi na kampuni zinazoshiriki katika maonesho ya mwaka huu ni ishara ya kuimarika kwa mazingira ya biashara na uwekezaji nchini. Ambapo, maarifa, teknolojia na lugha ya Kiswahili vinatajwa kuwa ni miongoni mwa nyenzo muhimu zitakazoifanya Tanzania kufikia malengo yake ya maendeleo.

Na. Timothy Mwakyenda – MAELEZO Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, amesema hali ya amani na usalama katika Jiji la Dar es Salaam ni shwari, huku akiwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere. Akizungumza wakati wa ziara ya kutembelea mabanda mbalimbali ya maonesho hayo leo Julai 7, 2026, Chalamila aliwapongeza wakazi wa Dar es Salaam kwa mwitikio mkubwa wa kushiriki maonesho hayo, akisema ushiriki huo unaonesha wananchi wanatumia vyema fursa ya kujifunza, kufanya biashara na kupata huduma mbalimbali zinazotolewa na washiriki. Alisema Serikali inaendelea kuhakikisha mazingira ya amani na utulivu yanatawala ili wananchi waweze kushiriki shughuli zao bila hofu, huku akiwataka kupuuza taarifa za upotoshaji zinazolenga kuwakatisha tamaa kushiriki maonesho hayo. Pokeeni salamu za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye anawapongeza kwa kazi nzuri mnazozifanya na sisi tunaendelea kuhamasisha Watanzania kutumia fursa hii muhimu ya kuona teknolojia mpya, kununua bidhaa kwa bei nafuu na kujifunza ubunifu mbalimbali unaooneshwa na washiriki kutoka ndani na nje ya nchi,” alisema Chalamila. Alibainisha kuwa maonesho ya mwaka huu yanayoadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake yamewakutanisha washiriki kutoka zaidi ya nchi 25, jambo linaloendelea kuimarisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha biashara, uwekezaji na ubunifu katika ukanda wa Afrika Mashariki. Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam SACP. Jumanne Muliro alisema hali ya usalama katika jiji hilo inaendelea kuwa tulivu, huku akieleza kuwa tathmini ya maeneo mbalimbali, ikiwemo Kibamba, Kimara, Ubungo, Manzese, Tegeta, Bunju na Kigamboni, inaonesha wananchi wanaendelea na shughuli zao za kila siku kwa amani. Aliwahakikishia wananchi kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kikamilifu kuhakikisha usalama unaendelea kuimarika katika kipindi chote cha maonesho hayo, na kuwataka waendelee kushirikiana na mamlaka kwa kutoa taarifa za viashiria vyovyote vinavyoweza kuhatarisha usalama. Muliro alisisitiza kuwa amani na utulivu ni msingi wa maendeleo ya taifa, akiwahimiza Watanzania kuendelea kuwa mabalozi wa amani kwa kushiriki shughuli za kijamii na kiuchumi kwa utulivu na uzalendo.

Na Mwandishi Wetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameiagiza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kupitia Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) na Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA), kwa kushirikiana na Balozi za Tanzania duniani, kuimarisha ufundishaji wa lugha ya Kiswahili na kuanzisha vituo vya utamaduni wa Kiswahili katika mataifa mbalimbali, ikiwemo Ufaransa. Maelekezo hayo yamewasilishwa leo, Julai 7, 2026, na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, wakati wa kufunga Maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani (MASKIDU 2026) yaliyofanyika katika Makao Makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), jijini Paris, Ufaransa. Kwa mujibu wa maelekezo ya Rais Samia, vituo hivyo vitakuwa kitovu cha kufundisha na kueneza lugha ya Kiswahili, kutangaza utamaduni wa Kitanzania na Afrika kwa ujumla, pamoja na kuimarisha diplomasia ya utamaduni. Vilevile, vitafungua fursa mpya za biashara, uwekezaji, utalii na ushirikiano wa kimataifa kupitia matumizi ya Kiswahili. Aidha, vituo hivyo vinatarajiwa kuwa sehemu muhimu ya kuwawezesha wananchi wa mataifa mbalimbali kujifunza historia, urithi, mila, desturi na ustaarabu wa Afrika kupitia lugha ya Kiswahili, ambayo inaendelea kupata hadhi na kutambuliwa katika majukwaa ya kimataifa. Katika hatua nyingine, Rais Samia amewahimiza Watanzania wanaoishi ughaibuni (Diaspora) kuhakikisha wanawarithisha watoto wao lugha ya Kiswahili ili kudumisha utambulisho wa Taifa, kuimarisha mshikamano wa kizazi hadi kizazi na kuhifadhi urithi wa kitamaduni wa Tanzania. Amesisitiza kuwa kadri Kiswahili kinavyoendelea kupanua wigo wake duniani, ndivyo kinavyozidi kuwa nyenzo muhimu ya kuimarisha ushawishi wa Tanzania kimataifa, kukuza utamaduni wa Kiafrika na kufungua fursa mpya za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Na Baraka Messa- MAELEZO Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema maonesho ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam ( Sabasaba) yameendelea kuwa daraja muhimu linalowaunganisha wazalishaji, wanunuzi, wafanyabiashara, masoko na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi. Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa maonesho hayo ya 50 Julai 3,2026 jijini Dares Salaam amesema maonesho hayo yamekuwa sehemu ya maisha ya Watanzania wengi, huku yakitoa fursa kwa wafanyabiashara wadogo kukua na kuwa wawekezaji wakubwa kupitia upatikanaji wa masoko na mitaji. “Kwa karibu miaka 50, maonesho ya Sabasaba yamekuwa daraja la kuwaunganisha wazalishaji, wanunuzi, wafanyabiashara, masoko na wawekezaji, huku yakiiunganisha Tanzania na dunia katika biashara na uwekezaji.” amesema. Amesema maonesho hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania kama kitovu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika, huku mafanikio hayo yakichangiwa na maboresho makubwa ya miundombinu na matumizi ya teknolojia yaliyofanywa na Serikali. Aidha, Rais Samia amesema diplomasia ya uchumi imeendelea kuzaa matunda ambapo katika mwaka uliopita mauzo ya bidhaa na huduma za Tanzania nje ya nchi yalifikia takribani dola za Marekani bilioni 17, sawa na ongezeko la asilimia 15 ikilinganishwa na kipindi kilichopita. Pia, mauzo ya dhahabu yaliongezeka kwa zaidi ya asilimia 35, yakionesha ukuaji wa sekta ya madini. Kwa upande wake Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mhe. Daniel Francisco Chapo, amesema Tanzania na Msumbiji zinapaswa kutumia historia yao ya ushirikiano kuimarisha uchumi wa kikanda kwa kubadilisha mipaka ya nchi hizo kuwa korido za maendeleo, biashara na uwekezaji badala ya kuwa vikwazo Amesema uchumi wa Tanzania na Msumbiji unakamilishana na una fursa kubwa ya kukuza minyororo ya thamani, biashara ya kikanda na uwekezaji kutokana na rasilimali nyingi, nguvu kazi ya vijana na nafasi ya kimkakati inayounganisha Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kupitia Bahari ya Hindi. Aidha, Rais Chapo amewataka wawekezaji wa ndani na nje ya Afrika waitazame Tanzania na Msumbiji kama washirika wa kuaminika wenye mazingira rafiki ya biashara, huku akisisitiza umuhimu wa kuwekeza katika viwanda, sayansi, ubunifu, uchumi wa kidijitali na akili Unde (AI).