Karibu!

Tunakukaribisha kwenye tovuti rasmi ya Msemaji Mkuu wa Serikali upate taarifa na habari sahihi zenye kuakisi malengo ya Serikali, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na matarajio ya Watanzania.

Mawasiliano

Tufuatilie

Na Josephina Lupasha – MAELEZO Kwa miaka mingi, wakazi wa Chamwino na maeneo jirani mkoani Dodoma wameishi na simulizi moja inayofanana; kuamka alfajiri kutafuta maji, kusubiri kwa saa nyingi kwenye foleni au kuishi kwa mgao wa maji usiotabirika. Leo, simulizi hiyo inaelekea kuwa historia kufuatia utekelezaji wa mradi mkubwa wa maji miji 28 Chamwino, unaotarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika huduma ya maji. Mradi huu wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 17 unatekelezwa katika Wilaya ya Chamwino na unatarajiwa kuhudumia wakazi wa kata za Chamwino, Msanga, Buigiri, Chinangali pamoja na maeneo ya karibu ikiwemo Mtumba na Ihumwa. Mradi huu ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kutekeleza miradi ya maji katika miji 28 Tanzania Bara, ukiwa na lengo la kuondoa changamoto ya upatikanaji wa maji na kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya uhakika. Ujenzi wa mradi ulianza Aprili mwaka 2023 na unatarajiwa kukamilika Agosti, 2026 ambapo hadi sasa, utekelezaji wake umefikia zaidi ya asilimia 74, huku baadhi ya maeneo tayari yakiwa yameanza kupata huduma ya maji. Kwa wakazi wa Chamwino, mradi huu si tu ujenzi wa miundombinu, bali ni ukombozi wa maisha yao ya kila siku. “Kiukweli, hapo nyuma maji hayakuwa yanatosha. Serikali imetukumbuka. Mradi mkubwa wa namna hii kwa sisi tuliopitia ugumu wa maji kwa muda mrefu ni jambo la kujivunia na la kushukuru sana,” anasema Bi. Maila Nyembela, mkazi wa Chamwino Ikulu. Licha ya mradi kutokamilika, tayari umeanza kuonesha matokeo chanya. Huduma ya maji sasa inapatikana kwa wastani wa saa 22 kwa siku, hali iliyopunguza kwa kiasi kikubwa mgao wa maji uliokuwa ukiwasumbua wakazi kwa miaka mingi. Kwa wanawake, ambao kwa muda mrefu walibeba jukumu kubwa la kutafuta maji, mradi huu umeleta matumaini mapya. “Awali tulilazimika kuamka alfajiri kutafuta maji au kununua kwa gharama kubwa. Ilikuwa tabu sana, hasa kwa wanawake. Kukamilika kwa mradi huu kutarahisisha maisha ya familia zetu na kutupa muda zaidi wa kushiriki shughuli za maendeleo,” anasema Bi. Mluka Michael, mkazi wa Chamwino. Mratibu Msaidizi wa Mradi huu kutoka Wizara ya Maji, Mhandisi Titho Alex, anaeleza kuwa mradi huo umejumuisha ujenzi wa visima virefu nane, matenki mawili ya kuhifadhi maji pamoja na miundombinu ya kutibu, kusukuma na kusambaza maji. Anasema tanki moja lililopo Chamwino Ikulu lina uwezo wa kuhifadhi maji lita 500,000 , huku lingine lililopo Msanga likiwa na uwezo wa kuhifadhi lita 200,000. “Mkakati huu utawezesha mradi kuzalisha lita milioni 12 za maji kwa siku, kiwango kitakachohakikisha wananchi wanapata huduma ya maji kwa saa 22 hadi 24 kila siku na kuondoa kabisa changamoto ya mgao wa maji Chamwino pamoja na kuimarisha huduma katika maeneo ya jirani,” anasema Mhandisi Alex. Kwa wananchi walioishi muda mrefu Chamwino, mradi huu ni ushahidi wa mabadiliko makubwa yanayoendelea kushuhudiwa katika Makao Makuu ya Nchi. “Nimeishi Dodoma tangu mwaka 1971. Wakati huo hatukuwa na maji kabisa. Baadaye yakaanza kupatikana lakini hayakutosha. Sasa karibu kila kitongoji kina maji, ingawa baadhi ya maeneo bado hupata kwa mgao. Tuna matumaini makubwa kwamba mradi huu ukikamilika tutapata maji kila siku. Hili ni jambo la kufurahisha sana,” anasema Mchungaji Anderson Ndoloji wa Mtaa wa Muungano. Meneja wa DUWASA Kanda ya Chamwino, Mhandisi Gray Mbalikila, anasema mradi huo utaongeza uwezo wa mamlaka hiyo kupanua huduma katika maeneo mapya yanayokua kwa kasi kutokana na ongezeko la wakazi, biashara na taasisi mbalimbali ndani ya Jiji la Dodoma. “Tunajivunia hatua tuliyofikia. Mradi huu ukikamilika, Chamwino itakuwa na akiba ya kutosha ya maji hata kwa ajili ya kata za jirani. Huduma itaongezeka kutoka kiwango cha sasa cha takribani asilimia 91 hadi kufikia asilimia 100,” anasema. Mbali na kuboresha upatikanaji wa maji, mradi huu unatarajiwa kuwa kichocheo cha maendeleo katika sekta mbalimbali. Upatikanaji wa maji ya uhakika utaimarisha afya za wananchi kwa kupunguza magonjwa yanayotokana na matumizi ya maji yasiyo salama, kuongeza usafi wa mazingira, kukuza biashara ndogo na shughuli za uzalishaji, pamoja na kuboresha huduma katika shule na vituo vya afya. Kadri Dodoma inavyoendelea kukua kama Makao Makuu ya Serikali, mahitaji ya huduma za msingi yanaongezeka. Mradi wa Maji Miji 28 Chamwino ni moja ya miradi ya kimkakati inayodhihirisha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma ya maji safi na salama. Kukamilika kwa mradi huu hakutakuwa tu mwisho wa changamoto ya muda mrefu ya upatikanaji wa maji kwa maelfu ya wananchi wa Chamwino na maeneo jirani, bali kutafungua ukurasa mpya wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi, ambapo maji yatakuwa si tena changamoto, bali chachu ya maendeleo.

■ Utekelezaji wake mbioni kukamilika ■ Wafanyabiashara wausubiri kwa hamu Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO Ule msemo wa Kiswahili unaosema “Mgeni njoo, mwenyeji apone” unaendelea kupata uhalisia kupitia ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato, mradi mkubwa unaotekelezwa na Serikali jijini Dodoma. Mbali na kuimarisha usafiri wa anga nchini, mradi huo tayari umeanza kuleta manufaa kwa wananchi kupitia ajira, biashara na fursa za uwekezaji, huku ukitarajiwa kuifanya Dodoma kuwa kitovu muhimu cha uchumi na usafiri wa anga. Mradi huo wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 370 unatarajiwa kukamilika Septemba 2026. Kwa sasa, ujenzi wa miundombinu umefikia asilimia 87.97, huku ujenzi wa majengo ukiwa umefikia asilimia 76.15. Ajira Zimefungua Milango ya Mafanikio Tangu ulipoanza mwaka 2022, mamia ya wakazi wa Dodoma wamepata ajira za muda na fursa za biashara zilizoongeza kipato cha familia zao. Mkazi wa Mpamaa, Maximilian Mwagike, ni mmoja wa wanufaika wa mradi huo. Anasema alianza kuuza miwa kwa kutumia baiskeli, lakini kuongezeka kwa shughuli za ujenzi kulipanua soko lake kiasi cha sasa kutumia guta kusafirisha bidhaa zake. “Biashara hii imenibadilisha maisha. Nimeboresha makazi yangu, ninalipia watoto wangu ada za shule binafsi na nimepanua biashara yangu,” anasema Mwagike, ambaye pia amepata ajira ya usimamizi wa mazingira katika mradi huo. Kwa upande wake, Mama Juma, aliyekuwa mama wa nyumbani, anasema mradi ulimwezesha kuanzisha biashara ya kupika na kuuza chakula kwa wafanyakazi wa ujenzi. “Leo naweza kulipia watoto wangu ada za shule, nimeweza kununua pikipiki inayoniingizia kipato na nina uhakika wa kuendelea na biashara hata baada ya mradi kukamilika,” anasema. Mradi Wajenga Ujuzi kwa Vijana Mbali na ajira za moja kwa moja, mradi huu umechangia kuwajengea vijana ujuzi na uzoefu wa kazi. Adam Kiula, anayefanya kazi katika kampuni inayosimika mifumo ya TEHAMA, kamera za usalama na mawasiliano, anasema amepata maarifa na uzoefu unaomuwezesha kushindana katika soko la ajira. Anawahimiza vijana kutumia kikamilifu fursa zinazotokana na miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali badala ya kusubiri ajira za kawaida. Wafanyabiashara Wanatazamia Mapinduzi ya Uchumi Faida za uwanja huo zinatarajiwa kuonekana zaidi baada ya kuanza kutoa huduma. Mfanyabiashara wa vifaa vya simu jijini Dodoma, anayefahamika kwa jina la Jeshi, anasema uwanja huo utarahisisha usafirishaji wa mizigo kutoka nje ya nchi na kupunguza gharama zinazotokana na kupitisha bidhaa kupitia Dar es Salaam. Naye mfanyabiashara wa bidhaa za urembo, Happiness Mgeani, anaamini kukamilika kwa uwanja huo kutapunguza hasara zinazotokana na ucheleweshaji na uhamishaji wa mizigo kutoka usafiri mmoja kwenda mwingine. Uwanja wa Hadhi ya Kimataifa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Dodoma, Mhandisi Zuhura Amani, anasema kazi zilizobaki ziko katika hatua za mwisho za ukamilishaji, zikiwemo ufungaji wa mifumo mbalimbali, taa za kuongozea ndege, alama za barabara za ndege na umaliziaji wa majengo. Anasema uwanja huo umejengwa kwa viwango vya kimataifa na utakuwa na uwezo wa kupokea ndege kubwa kama Airbus A330 na Boeing 787 Dreamliner, pamoja na kuhudumia (maegesho) ndege 17 kwa wakati mmoja. Aidha, anaeleza kuwa uwanja huo utakuwa na mnara wa kisasa wa kuongozea ndege wenye urefu wa mita 56.2, mnara wa pili kwa urefu Afrika Mashariki, pamoja na maeneo ya biashara, maegesho ya magari na nafasi ya upanuzi wa baadaye. Maandalizi ya Uendeshaji Yamekamilika Kwa upande wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mhandisi Zacharo Mduma amesema maandalizi ya kuanza uendeshaji wa uwanja huo yanaendelea, ikiwa ni pamoja na kuandaa watumishi watakaotoa huduma za uhamiaji, forodha, afya, usalama na zimamoto mara baada ya mradi kukabidhiwa rasmi. Lango Jipya la Ukuaji wa Uchumi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato unatarajiwa kuwa wa Daraja F, kiwango cha juu kinachotambulika kimataifa. Mradi huo umefadhiliwa kwa asilimia 85 na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), huku Serikali ya Tanzania ikichangia asilimia 15. Baada ya kukamilika, uwanja huo unatarajiwa kuhudumia zaidi ya abiria milioni 1.5 kwa mwaka na kuwa lango jipya la biashara, utalii na uwekezaji. Zaidi ya miundombinu ya usafiri, Uwanja wa Ndege wa Msalato unatajwa kuwa kichocheo cha ukuaji wa uchumi wa Dodoma na Taifa kwa ujumla, huku ukiendelea kuthibitisha kwamba miradi mikubwa ya maendeleo inaweza kubadili maisha ya wananchi hata kabla haijakamilika.

Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), limeidhinisha kutolewa mara moja kwa takriban dola za Marekani milioni 443.9 kwa Tanzania baada ya kukamilisha tathmini za mwisho chini ya programu za Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na Resilience and Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Katika taarifa iliyotolewa Julai 10, IMF imesema uamuzi huo unafuatia kukamilika kwa mapitio ya sita na saba ya mpango wa ECF pamoja na mapitio ya tatu na nne ya mpango wa RSF, ambapo fedha hizo zinajumuisha takriban dola za Marekani milioni 158.75 chini ya ECF na dola za Marekani milioni 298.37 chini ya RSF. IMF imeeleza kuwa uchumi wa Tanzania umeendelea kuonyesha uimara, huku ukuaji wa Pato la Taifa ukifikia asilimia 5.9 mwaka 2025 na kutarajiwa kufika karibu asilimia 6.2 kwa muda wa kati. Sekta zilizotajwa kuchangia matarajio hayo ni pamoja na madini, kilimo na utalii. Kwa mujibu wa tathmini hiyo, Tanzania imeendelea kudumisha utulivu wa uchumi mpana na mfumuko wa bei umebaki chini, ukiwa asilimia 4.0 mwezi Juni 2026. Hata hivyo, IMF imeonya kuwa kupanda kwa bei za mafuta duniani kunaendelea kutoa shinikizo kwa gharama za maisha na uchumi kwa ujumla. Taarifa hiyo imeonyesha pia kuwa utekelezaji wa mpango wa mageuzi ya kiuchumi kwa ujumla ulikuwa wa kuridhisha. Vigezo vingi vya utendaji vilifikiwa kwa wakati, ingawa baadhi ya malengo na mageuzi, hasa katika maeneo ya nishati, usimamizi wa VAT, utawala wa Benki Kuu na uwekezaji wa umma, yalichelewa au hayakukamilika kama ilivyotarajiwa. Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa IMF na Kaimu Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Bw. Bo Li, alisema Tanzania imefanikiwa kuhifadhi utulivu wa uchumi licha ya misukosuko ya ndani na nje. Alisema hatua zaidi zinahitajika katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani, kuboresha usimamizi wa fedha za umma, na kuongeza uwekezaji katika sekta muhimu kama elimu na afya. Aidha, IMF imeishauri Tanzania kuendelea na mageuzi ya kuboresha mazingira ya biashara, kuimarisha sekta binafsi, na kuongeza uwezo wa nchi kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Shirika hilo limeonya kuwa kuendelea kwa mzozo wa Mashariki ya Kati kunaweza kudhoofisha ukuaji wa uchumi na kuongeza mfumuko wa bei. Pamoja na mtazamo chanya wa uchumi, IMF imesisitiza kuwa Tanzania bado inakabiliwa na changamoto kubwa za kupunguza umaskini, kufikia malengo ya maendeleo endelevu, na kuandaa fursa za kutosha kwa idadi ya watu inayotarajiwa kuongezeka maradufu ifikapo mwaka 2050. Kwa ujumla, uamuzi wa IMF unaonekana kuwa ishara ya kuendelea kwa imani ya taasisi hiyo kwa mwenendo wa uchumi wa Tanzania, huku ukitoa msukumo mpya kwa Serikali kuharakisha mageuzi na kuimarisha ustahimilivu wa uchumi. Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) ameshukuru uamuzi huo wa Taasisi hiyo kubwa ya Fedha duniani (IMF), kwa kuendelea kuamini mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii ambayo nchi imeendelea kupiga hatua kubwa hadi sasa na kuungwa mkono na IMF. Tanzania imekuwa na ushirikiano wa muda mrefu na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) tangu ilipojiunga na IMF tarehe 10 Septemba 1962, ambapo jumla ya ahadi ya mikopo na misaada ya IMF kwa Tanzania imefikia Dola ya Marekani bilioni 4.578. Kati ya kiasi hicho, portfolio hai ya sasa ni dola za Marekani bilioni 2.52.

Na. Timothy Mwakyenda – MAELEZO Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Ithibati ya Maisha utakaowezesha waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango mkubwa katika maendeleo ya tasnia ya habari nchini kutambuliwa rasmi, licha ya kutokukidhi vigezo vya kielimu vilivyowekwa na Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016. Uzinduzi wa mwongozo huo umetajwa kuwa hatua muhimu ya kutambua mchango wa wanahabari waliolitumikia taifa kwa uadilifu na weledi kwa miaka mingi kabla ya kuanza kutumika kwa masharti mapya ya kitaaluma yanayomtaka mwandishi wa habari kuwa na angalau stashahada (Diploma) ya uandishi wa habari. Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya JAB, uliofanyika Julai 11, 2026 katika kijiji cha Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo katika viwanja vya Maonesho ya 50 ya kimataifa ya biashara Dar es salaam (sabasaba) Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Tildo Mhando, kupitia taarifa iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, alisema mwongozo huo unalenga kuwapa Ithibati ya Maisha waandishi wa habari wakongwe ambao wakati Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ilipopitishwa mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari. Alieleza kuwa waandishi hao hawakupata fursa ya kusomea darasani hadi kufikia kiwango cha diploma, lakini walijijengea uwezo kupitia uzoefu na walishiriki kwa kiwango kikubwa katika maendeleo ya vyombo vya habari na ujenzi wa taifa. “Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa kizazi cha mwanzo na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma hii” ilisisitiza taarifa hiyo. Aidha, aliishukuru Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kushirikiana na JAB katika kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari na kusisitiza umuhimu wa weledi, uwajibikaji na maadili kwa waandishi wa habari nchini. Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi wa JAB, Bwana Patrick Kipangula alisema kuwa uzinduzi wa Mwongozo wa Ithibati ya Maisha ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya kuhakikisha kuwa ni pamoja na kuimarisha viwango vya taaluma kupitia sheria, mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia taifa kwa uaminifu na uzalendo unaendelea kutambuliwa na kuthaminiwa.

Na Adelina Johnbosco – MAELEZO Barabara za Mzunguko Jijini Dodoma imechangia kwa kiasi kikubwa kuondoa msongamano wa magari katikati ya jiji, hususan magari makubwa ya mizigo ya ndani na yanayokwenda nchi za nje. Mradi huu wa barabara ya njia nne kwa kiwango cha lami una urefu wa jumla ya kilometa 112.3 huku sehemu ya kwanza (lot 1) yenye kilometa 52.3 ikiwa imekamilika kwa asilimia 93.3. Barabara hii imeunganisha barabara kuu za mikoa minne, bandari kavu Ihumwa – Morogoro, Veyula – Arusha, Nala – Singida na Matumbulu – Iringa ambako sehemu ya pili ya ujenzi (lot 2) inaanzia. Shughuli za usafiri na usafirishaji tayari zimeanza katika barabra hiyo, watumiaji wanashuhudia urahisi wa safari kutokana na kutokuwepo foleni.  Imeturahisishia sana, inafanya safari iwe fupi kutokana na ukweli kwamba njia hii haina foleni hata kidogo kama kule mjini kati, mwanzoni kutoka Ihumwa hadi Nala ilikuwa tunatumia takribani saa na nusu hata zaidi, lakini kwa sasa tunatumia dakika 45 hadi 48 kwa safari hiyo hiyo” Bw. Simon Ndamanyilu, dereva lori Akitoa ufafanuzi kuhusu barabara hiyo hivi karibuni, Mhandisi Morice Mlay, kutoka kampuni ya mzawa ya  Inter-Consult Ltd (Mhandisi Mshauri wa Mradi), amesema barabara hiyo tayari imeanza kutumika na inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Oktoba, 2026 ambapo itakuwa imekamilika kabisa. “Ujenzi sehemu ya kwanza umefikia ukingoni, bado baadhi ya vitu vichache sana ikiwemo taa za barabarani na umaliziaji wa njia za watembea kwa miguu, magari mengi yanapita na yanapata urahisi kwa sababu hakuna foleni kwenye njia hii, mfano magari yanatoka moja kwa moja kutoka eneo la mzunguko wa Ihumwa hadi Nala ile barabara inayounganisha barabara ya Iringa bila kusimama popote” ametanabaisha Mha. Mlay Barabara hiyo ya njia nne yenye njia mbili kila upande, zimetenganishwa na uwazi katikati kwa ajili ya matumizi mengine pindi itakapohitajika kuongeza miundombinu mingine au uboreshaji. “Kuna baadhi ya watu wanashangaa kuhusu hili tuta lililoachwa katikati, hili ni kwa ajili ya matumizi ya baadaye mfano ujenzi wa barabara za mwendo kasi au kitu chochote kitakachoamuliwa kufanyika, lengo kuu ni kuepuka kutobomoa barabara kwa ajili ya kufanya kitu kipya” – Mha. Mlay  Baadhi ya wananchi jijini Dodoma wanaonesha furaha yao kutokana na uwepo wa barabara hiyo mpya inayopitisha magari mengi hasa magari makubwa ya mizingo kwenda ndani na nje ya nchi kwa wakati mmoja. Kwa mujibu wa Mha. Mlay, yapo magari yanayoelekea nchini Rwanda, Congo na Burundi kupitia barabara ya mzunguko. Katika eneo la Nala ambako kuna mojawapo ya makutano ya barabara hiyo na sehemu ya maegesho ya magari, wakazi wa maeneo hayo wamepata fursa ya kufanya biashara kutokana na uwepo wa watu wengi kwa wakati mmoja. “Kituo hiki yanapitisha na kusimama magari ya kila aina, hii ni tofauti na mwanzo, magari yakisimama hapa watu wanashuka na wengine wanakuwa wamesubiria kupanda, wengine ni madereva wa magari makubwa, kwa hiyo lazima watahitaji kupata mahitaji kutoka kwetu hasa chakula, hii ni furaha kwetu” Mary John, mama ntilie Tamanio la wengi ni kuona barabara inaanza kazi rasmi kwani kwao ni tegemeo mojawapo la njia ya kuongeza kipato. Kama kwa sasa nauza bidhaa zangu kwa kiwango ambacho naona kinafaa, nawaza kwamba barabara hii ikianza kutumika rasmi magari yataongezeka, yataegeshwa kwa wingi zaidi na watu watakuwa wengi kuliko hivi” amesema Bi. Veronica Alfred, muuza nafaka eneo la Nala. Mussa Rajab mkazi wa Nala na mkuli eneo hilo, akiwawakilisha wabeba mizigo wenzake, anasema uwepo wa sehemu ya kisasa ya kuegesha magari umefanya kazi yao kuwa rahisi na kukuza kipato. “Mwanzoni eneo hili halikuwepo, hivyo kusimama kwa magari hapa ilitegemea udharura wa dereva hapo na sisi tunavizia kubeba mizigo japo kwa uchache sana, siku hizi magari yanasimama na mizigo inateremshwa hivyo tunabeba na kupata riziki” – Bw. Rajab Mradi huu kipande cha kwanza utagharimu shilingi bil. 100.84 hadi kukamilika kwake, na unatarajiwa kuwa mwarobaini wa msongamano wa magari katikati ya jiji pia kukuza uchumi wa mkoa wa Dodoma, mikoa ya jirani na nchi kwa ujumla.

Na Timothy Mwakyenda – MAELEZO Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali amesema kuwa mafanikio ya Tamasha la Lugha ya Kiswahili lililofanyika nchini Ufaransa yamefungua ukurasa mpya wa kuitangaza lugha ya Kiswahili duniani na kuifanya kuwa nyenzo muhimu ya kukuza uchumi, biashara na diplomasia ya Tanzania. Akizungumza Julai 8, 2026, alipotembelea Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), Msigwa amesema kuwa ushiriki wa Tanzania katika tamasha hilo umeonyesha kuwa Kiswahili sasa si lugha ya mawasiliano pekee, bali ni rasilimali yenye uwezo wa kufungua fursa za kiuchumi kwa Watanzania.   Msigwa ameendelea kusema kuwa mataifa mengi yaliyofanikiwa kiuchumi yamenufaika pia kwa kutumia lugha zao kama chachu ya biashara na ubunifu, hivyo Watanzania wanapaswa kukitumia Kiswahili kama nyenzo ya kutangaza bidhaa, huduma na utamaduni wao katika soko la kimataifa. ” Baada ya mafanikio ya tamasha hilo, taasisi za Serikali na sekta binafsi zinapaswa kujipanga kimkakati ili kutumia fursa zinazotokana na kuongezeka kwa matumizi ya Kiswahili duniani, hatua itakayochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yenye lengo la kujenga uchumi wa dola za Marekani trilioni moja”, amesisitiza Msigwa. Akihusisha ujumbe huo na Maonesho ya Sabasaba, Msigwa amefafanua kuwa maonesho hayo yanatoa jukwaa muhimu la kuhamasisha uzalishaji wa bidhaa za ndani, ubunifu wa teknolojia na uongezaji thamani wa mazao, akitaja mfano wa vijana wa DIT ambao wametengeneza bajaji ya umeme na wafanyabiashara wanaochakata mazao kama korosho na parachichi na kusisitiza kuwa maendeleo hayo yanapaswa kuungwa mkono ili kuongeza ajira, kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje na kuhakikisha fedha nyingi zaidi zinabaki kuzunguka ndani ya uchumi wa Tanzania. Aidha, amewataka Watanzania kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi kwa kuelekeza nguvu katika uzalishaji, biashara, kilimo, viwanda na ubunifu badala ya kushawishiwa na ajenda zinazoweza kuvuruga maendeleo ya Taifa. Sambamba na hilo amewahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya Sabasaba ili kujifunza teknolojia mpya, kupata maarifa kutoka kwa washiriki wa ndani na nje ya nchi na kutumia fursa hizo kuboresha shughuli zao za kiuchumi huku akibainisha kuwa ongezeko la idadi ya nchi na kampuni zinazoshiriki katika maonesho ya mwaka huu ni ishara ya kuimarika kwa mazingira ya biashara na uwekezaji nchini. Ambapo, maarifa, teknolojia na lugha ya Kiswahili vinatajwa kuwa ni miongoni mwa nyenzo muhimu zitakazoifanya Tanzania kufikia malengo yake ya maendeleo.

Na. Timothy Mwakyenda – MAELEZO Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, amesema hali ya amani na usalama katika Jiji la Dar es Salaam ni shwari, huku akiwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere. Akizungumza wakati wa ziara ya kutembelea mabanda mbalimbali ya maonesho hayo leo Julai 7, 2026, Chalamila aliwapongeza wakazi wa Dar es Salaam kwa mwitikio mkubwa wa kushiriki maonesho hayo, akisema ushiriki huo unaonesha wananchi wanatumia vyema fursa ya kujifunza, kufanya biashara na kupata huduma mbalimbali zinazotolewa na washiriki. Alisema Serikali inaendelea kuhakikisha mazingira ya amani na utulivu yanatawala ili wananchi waweze kushiriki shughuli zao bila hofu, huku akiwataka kupuuza taarifa za upotoshaji zinazolenga kuwakatisha tamaa kushiriki maonesho hayo. Pokeeni salamu za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye anawapongeza kwa kazi nzuri mnazozifanya na sisi tunaendelea kuhamasisha Watanzania kutumia fursa hii muhimu ya kuona teknolojia mpya, kununua bidhaa kwa bei nafuu na kujifunza ubunifu mbalimbali unaooneshwa na washiriki kutoka ndani na nje ya nchi,” alisema Chalamila. Alibainisha kuwa maonesho ya mwaka huu yanayoadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake yamewakutanisha washiriki kutoka zaidi ya nchi 25, jambo linaloendelea kuimarisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha biashara, uwekezaji na ubunifu katika ukanda wa Afrika Mashariki. Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam SACP. Jumanne Muliro alisema hali ya usalama katika jiji hilo inaendelea kuwa tulivu, huku akieleza kuwa tathmini ya maeneo mbalimbali, ikiwemo Kibamba, Kimara, Ubungo, Manzese, Tegeta, Bunju na Kigamboni, inaonesha wananchi wanaendelea na shughuli zao za kila siku kwa amani. Aliwahakikishia wananchi kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kikamilifu kuhakikisha usalama unaendelea kuimarika katika kipindi chote cha maonesho hayo, na kuwataka waendelee kushirikiana na mamlaka kwa kutoa taarifa za viashiria vyovyote vinavyoweza kuhatarisha usalama. Muliro alisisitiza kuwa amani na utulivu ni msingi wa maendeleo ya taifa, akiwahimiza Watanzania kuendelea kuwa mabalozi wa amani kwa kushiriki shughuli za kijamii na kiuchumi kwa utulivu na uzalendo.

Na Mwandishi Wetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameiagiza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kupitia Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) na Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA), kwa kushirikiana na Balozi za Tanzania duniani, kuimarisha ufundishaji wa lugha ya Kiswahili na kuanzisha vituo vya utamaduni wa Kiswahili katika mataifa mbalimbali, ikiwemo Ufaransa. Maelekezo hayo yamewasilishwa leo, Julai 7, 2026, na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, wakati wa kufunga Maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani (MASKIDU 2026) yaliyofanyika katika Makao Makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), jijini Paris, Ufaransa. Kwa mujibu wa maelekezo ya Rais Samia, vituo hivyo vitakuwa kitovu cha kufundisha na kueneza lugha ya Kiswahili, kutangaza utamaduni wa Kitanzania na Afrika kwa ujumla, pamoja na kuimarisha diplomasia ya utamaduni. Vilevile, vitafungua fursa mpya za biashara, uwekezaji, utalii na ushirikiano wa kimataifa kupitia matumizi ya Kiswahili. Aidha, vituo hivyo vinatarajiwa kuwa sehemu muhimu ya kuwawezesha wananchi wa mataifa mbalimbali kujifunza historia, urithi, mila, desturi na ustaarabu wa Afrika kupitia lugha ya Kiswahili, ambayo inaendelea kupata hadhi na kutambuliwa katika majukwaa ya kimataifa. Katika hatua nyingine, Rais Samia amewahimiza Watanzania wanaoishi ughaibuni (Diaspora) kuhakikisha wanawarithisha watoto wao lugha ya Kiswahili ili kudumisha utambulisho wa Taifa, kuimarisha mshikamano wa kizazi hadi kizazi na kuhifadhi urithi wa kitamaduni wa Tanzania. Amesisitiza kuwa kadri Kiswahili kinavyoendelea kupanua wigo wake duniani, ndivyo kinavyozidi kuwa nyenzo muhimu ya kuimarisha ushawishi wa Tanzania kimataifa, kukuza utamaduni wa Kiafrika na kufungua fursa mpya za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Na Baraka Messa- MAELEZO Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema maonesho ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam ( Sabasaba) yameendelea kuwa daraja muhimu linalowaunganisha wazalishaji, wanunuzi, wafanyabiashara, masoko na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi. Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa maonesho hayo ya 50 Julai 3,2026 jijini Dares Salaam amesema maonesho hayo yamekuwa sehemu ya maisha ya Watanzania wengi, huku yakitoa fursa kwa wafanyabiashara wadogo kukua na kuwa wawekezaji wakubwa kupitia upatikanaji wa masoko na mitaji. “Kwa karibu miaka 50, maonesho ya Sabasaba yamekuwa daraja la kuwaunganisha wazalishaji, wanunuzi, wafanyabiashara, masoko na wawekezaji, huku yakiiunganisha Tanzania na dunia katika biashara na uwekezaji.” amesema. Amesema maonesho hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania kama kitovu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika, huku mafanikio hayo yakichangiwa na maboresho makubwa ya miundombinu na matumizi ya teknolojia yaliyofanywa na Serikali. Aidha, Rais Samia amesema diplomasia ya uchumi imeendelea kuzaa matunda ambapo katika mwaka uliopita mauzo ya bidhaa na huduma za Tanzania nje ya nchi yalifikia takribani dola za Marekani bilioni 17, sawa na ongezeko la asilimia 15 ikilinganishwa na kipindi kilichopita. Pia, mauzo ya dhahabu yaliongezeka kwa zaidi ya asilimia 35, yakionesha ukuaji wa sekta ya madini. Kwa upande wake Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mhe. Daniel Francisco Chapo, amesema Tanzania na Msumbiji zinapaswa kutumia historia yao ya ushirikiano kuimarisha uchumi wa kikanda kwa kubadilisha mipaka ya nchi hizo kuwa korido za maendeleo, biashara na uwekezaji badala ya kuwa vikwazo Amesema uchumi wa Tanzania na Msumbiji unakamilishana na una fursa kubwa ya kukuza minyororo ya thamani, biashara ya kikanda na uwekezaji kutokana na rasilimali nyingi, nguvu kazi ya vijana na nafasi ya kimkakati inayounganisha Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kupitia Bahari ya Hindi. Aidha, Rais Chapo amewataka wawekezaji wa ndani na nje ya Afrika waitazame Tanzania na Msumbiji kama washirika wa kuaminika wenye mazingira rafiki ya biashara, huku akisisitiza umuhimu wa kuwekeza katika viwanda, sayansi, ubunifu, uchumi wa kidijitali na akili Unde (AI).