Karibu!

Tunakukaribisha kwenye tovuti rasmi ya Msemaji Mkuu wa Serikali upate taarifa na habari sahihi zenye kuakisi malengo ya Serikali, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na matarajio ya Watanzania.

Mawasiliano

Tufuatilie

Kituo Cha Habari

Na Baraka Messa – MAELEZO Serikali imekamilisha hatua muhimu za kisheria zitakazowezesha kuanza kwa malipo ya kifuta jasho kwa askari waliojitolea kushiriki Vita ya Kagera dhidi ya utawala wa Idd Amin mwaka 1978/79 ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wao katika kulinda uhuru na usalama wa Taifa. Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba akijibu maswali ya papo kwa papo Juni, 18, 2026, bungeni Dodoma, amesema kuwa vikwazo vya kisheria vilivyokuwa vinazuia utekelezaji wa malipo hayo vimeondolewa kufuatia maelekezo ya Rais, hivyo kufungua njia kwa askari hao kupata stahiki zao baada ya kusubiri kwa muda mrefu. Akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Njombe, Mhe. Deo Mwanyika, Mhe. Waziri Mkuu, amesema kuwa Serikali inaendelea na zoezi la utambuzi na uhakiki wa askari hao, ambapo takribani askari 7,200 wanatarajiwa kunufaika na mpango huo mara baada ya taratibu husika kukamilika. Hatua hii ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya kuthamini na kutambua mchango wa wananchi walioweka maisha yao rehani katika nyakati muhimu za historia ya Taifa. Mwaka 2025 Serikali ilikamilisha zoezi la kuwatambua baadhi ya washiriki wa vita hii kutoka Uganda waliokuwa na mchango katika harakati za kuikomboa nchi wakati wa Vita vya Kagera, hatua iliyoweka msingi wa kuendelea kuwathamini wote walioshiriki katika mapambano hayo,” amesema Mhe. Waziri Mkuu. Vita ya Kagera ya mwaka 1978/79 inabaki kuwa moja ya matukio muhimu katika historia ya Tanzania na Afrika Mashariki, ambapo majeshi ya Tanzania kwa kushirikiana na wapigania uhuru wa Uganda yaliweza kuondoa utawala wa Idd Amin na kurejesha usalama katika eneo hilo.  

Na. Mwandishi Wetu – Singida Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Waziri wa Maji kwenda Mkoa wa Mwanza kushughulikia mara moja changamoto ya upatikanaji wa maji inayowakabili wananchi wa mkoa huo na kuhakikisha huduma hiyo inarejea kwa haraka. Dkt. Mwigulu ametoa maelekezo hayo Juni 14, 2026 alipokuwa akizungumza, kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi wa Tarafa ya Kiomboi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Lulumba, Wilaya ya Iramba mkoani Singida. Amesema amepokea taarifa kuhusu changamoto ya maji katika Mkoa wa Mwanza na tayari amemuelekeza Waziri mwenye dhamana ya maji kwenda eneo husika kusimamia upatikanaji wa suluhisho la haraka.  Nimemtuma Waziri aende haraka Mwanza akasimamie jambo lile mpaka maji yapatikane. Sisi watu wa Singida tunataka tupate maji toka Mwanza. Simiyu tunataka tupate maji toka Mwanza. Dodoma tunataka tupate maji toka Mwanza. Tabora, wengine wameshaanza kupata maji toka Mwanza. Leo kuja kuambiwa Mwanza, pale pale lilipo Ziwa Victoria, pana shida ya maji. Hili ni jambo ambalo haliwezi kueleweka, na wala hatuwezi kulielewa,” amesema Dkt. Mwigulu. Amesema hakuna sababu ya wananchi kuendelea kukosa huduma hiyo wakati chanzo cha maji kinajulikana na miundombinu ya mradi ipo.  “Hatutaki ngonjera za maneno. Hawa wanasema si bomba limekuwaje, hawa wanasema si umeme umekuwaje. Chanzo sisi tunajua kiko pale, hatuna shida ya chanzo cha maji, na mradi upo, na maji yapo. Haya mambo mengine ni ya ngonjera, mimi sitaki kuyasikia,” amesema. Waziri Mkuu amewataka wataalamu wa sekta ya maji pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kufanya kazi kwa pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa haraka. “Mkuu wa Mkoa awatafute wataalamu wake, awatafute TANESCO na wataalamu wa maji. wachimbe kiini cha tatizo na wakeshe mpaka wananchi wapate maji. Kunapopambazuka kesho nipate majawabu kwamba maji yamepatikana,” amesema. Juni 9, 2026, Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) ilitoa taarifa kwa umma kuhusu upungufu wa huduma ya maji uliosababishwa na hitilafu za umeme zilizokuwa zikijitokeza mara kwa mara. Wakati huohuo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imejipanga kuhakikisha changamoto ya upatikanaji wa maji katika Tarafa ya Kiomboi na maeneo mengine ya Wilaya ya Iramba inapata ufumbuzi wa kudumu kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji pamoja na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta hiyo nchini. Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele maalum katika sekta ya maji kwa kutekeleza miradi ya kimkakati inayolenga kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi.  Niwahakikishie kwamba hili ni eneo ambalo Mheshimiwa Rais ameliwekea kipaumbele cha hali ya juu kwa sababu maji ni uhai, maji ni maisha. Tulihangaika kupata chanzo cha uhakika cha maji na sasa kimepatikana, hatua mbalimbali zinaendelea ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa uhakika,” amesema. Aidha, amesema Serikali inaendelea na utekelezaji wa mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji pamoja na kuimarisha uwezo wa uchimbaji wa visima, ujenzi wa mabwawa na upimaji wa vyanzo vya maji ili kukabiliana na changamoto ya maji katika maeneo mbalimbali nchini. Dkt. Mwigulu ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi amesema Serikali inaendelea na usanifu wa barabara ya Kiomboi–Kisiriri–Sibiti kwa lengo la kuijenga kwa kiwango cha lami na kuboresha mawasiliano kati ya wananchi wa maeneo hayo na maeneo jirani. Aidha, amesema usanifu wa barabara ya Kitusha–Galangala–Kisana–Kinampanda–Kisiriri umekamilika, huku Serikali ikiendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mingine ya barabara katika Wilaya ya Iramba ili kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi. Pia amesema usanifu wa daraja la kuunganisha eneo la Hospitali ya Kiomboi na maeneo ya Meli pamoja na Iguguno umekamilika na hatua zinazofuata ni kumpata mkandarasi kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huo. Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya kuanzisha Chuo Kikuu katika eneo la Kiomboi baada ya eneo lililotengwa kuridhiwa na wataalamu husika.  Hapa Kiomboi tutakuwa na Chuo Kikuu. Eneo limekaguliwa na kuridhiwa na hatua za utekelezaji zinaanza,” amesema. Amesema pindi ujenzi wake utakapokamilika, Chuo Kikuu hicho kinatarajiwa kuanza kwa awamu ya kwanza kwa uwezo wa kuhudumia wanafunzi takribani 10,000.

Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imeandika historia nyingine baada ya jopo la madaktari bingwa na wataalamu wa afya kufanikisha salama uzazi wa watoto watano kwa wakati mmoja kwa Bi. Victoria Mkwizu, mkazi wa Tabata jijini Dar es Salaam. Watoto hao ambao watatu ni wa kiume na wawili ni wa kike, wamezaliwa tarehe 13 Juni 2026 na wanaendelea vizuri chini ya uangalizi wa wataalamu wa hospitali hiyo. Akiwa wodini, Bi. Victoria amesema anafurahia huduma alizopata katika hospitali hiyo tangu alipopokelewa hadi kujifungua. “Nawapongeza madaktari, wauguzi na wataalamu wengine wa afya kwa uangalizi wa karibu walionipatia katika kipindi chote cha matibabu kwani mchango wao umetuwezesha mimi na watoto kuendelea vizuri”, amesema Bi. Victoria. Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji, Dkt. Rachel Mhaville amesema tukio hilo ni la kipekee na limehitaji ufuatiliaji wa karibu kutoka kwa timu ya wataalamu wa hospitali hiyo ili kuhakikisha usalama wa mama na watoto huku akimpongeza Bi. Victoria kwa kujifungua salama na kuwatakia wote afya njema. Tunampongeza sana Bi. Veronica kwa kubarikiwa watoto mapacha watano, hospitali yetu itagharamia gharama zote za matibabu za kwake na watoto wake kuanzia alipolazwa hospitalini tarehe 15 Mei, 2026 hadi watakapomaliza matibabu na kuruhusiwa kurejea nyumbani”, ameeleza Dkt. Rachel. Amefafanua kuwa, hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za hospitali kuhakikisha mama na watoto wanaendelea kupata huduma bora na salama katika kipindi hicho.

Na. Timothy Mwakyenda – MAELEZO.  Serikali imebainisha mikakati mipya ya kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani katika mwaka wa fedha 2026/2027, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa taifa kujitegemea kiuchumi na kugharamia maendeleo kupitia rasilimali zake. Akizungumza Bungeni jijini Dodoma Juni 11, 2026 wakati akiwasilisha Bajeti ya Serikali ya mwaka 2026/2027, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, amesema Serikali imejipanga kuongeza kasi ya juhudi za kujitegemea kiuchumi kwa kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani na kuziba mianya yote ya upotevu wa mapato ya Serikali. “Ni muhimu kuendelea kuimarisha uwezo wa nchi kugharamia maendeleo yake kwa kutumia vyanzo vya ndani vya mapato ili kupunguza utegemezi wa mikopo na changamoto zake,” amesema Balozi Omary. Amefafanua kuwa kupitia Mkakati wa Ukusanyaji wa Mapato wa Muda wa Kati wa mwaka 2025/26 hadi 2027/28, Serikali itaanza kutekeleza hatua mbalimbali zitakazopanua wigo wa kodi na kuongeza mapato ya ndani. Miongoni mwa hatua hizo ni kuvutia uwekezaji wa ndani na nje ya nchi ili kuongeza shughuli za kiuchumi, ajira na mapato ya kodi. Serikali pia itaendelea kuhamasisha ulipaji kodi kwa hiari kupitia majukwaa ya mazungumzo kati ya Serikali na sekta binafsi pamoja na kuimarisha matumizi ya mashine za kutolea risiti za kielektroniki (EFD). Aidha, Waziri Omar amesema Serikali itaboresha mifumo ya TEHAMA inayosimamia mapato kwa kutumia teknolojia za kisasa ikiwemo uchambuzi wa taarifa kubwa (Big Data), sambamba na kuunganisha mifumo mbalimbali ya Serikali ili kuongeza uwazi, ufanisi na tija katika ukusanyaji wa mapato. Pia, amesema Serikali itaongeza usimamizi wa taasisi za umma ili ziweze kuchangia zaidi mapato ya Serikali kupitia gawio na michango inayowasilishwa kwa wakati katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Katika hatua nyingine, Serikali itaanza kutekeleza baadhi ya mapendekezo 284 yaliyotolewa na Tume ya Rais ya Kuboresha Mfumo wa Kodi. Vilevile, bidhaa zote zinazozalishwa nchini zitatakiwa kuwa na misimbo pau (barcode) kwa lengo la kurahisisha ufuatiliaji wa bidhaa na kudhibiti upotevu wa mapato. Balozi Omar ametangaza pia kuanzishwa kwa programu mpya ya “Tuzo za Uzalendo” itakayozinduliwa rasmi Julai ,2026 kwa lengo la kuhamasisha wananchi kudai risiti na wafanyabiashara kutoa risiti kwa hiari kupitia mfumo wa risiti za kielektroniki na droo za bahati nasibu. Amesema hatua hiyo inalenga kujenga utamaduni wa uzalendo katika ulipaji wa kodi, kuongeza ushiriki wa wananchi katika kulinda mapato ya taifa na kuimarisha uwajibikaji katika shughuli za biashara pia kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato, kupunguza utegemezi wa mikopo na kuimarisha msingi wa uchumi unaojitegemea, shindani na wenye uwezo mkubwa wa kugharamia maendeleo ya wananchi.