Kituo Cha Habari

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amemuasili mtoto mchanga wa kike leo tarehe 11 Machi, 2026, katika makazi yake, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma. Mtoto huyo aliyepewa jina la Grace Samia Suluhu, alitelekezwa mjini Nzega, mkoani Tabora, na amekabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia na Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai. Akizungumza wakati wa kumkabidhi mtoto huyo, Mkuu wa Wilaya Tukai alisema mtoto huyo aliokotwa tarehe 17 Januari, 2026 akiwa ametelekezwa katika eneo jirani na nyumba ya wageni ya Kasulu, Nzega Mjini. Alieleza kuwa baada ya kupokea taarifa hizo, alishirikiana na Jeshi la Polisi kumchukua mtoto huyo na kumpeleka hospitalini kwa uchunguzi na uangalizi, huku juhudi za kumtafuta mama yake zikiendelea bila mafanikio. Rais Dkt. Samia amemkaribisha mtoto huyo katika familia yake na kuahidi kumpatia malezi, ulinzi na huduma zote muhimu ili akue katika mazingira salama na yenye upendo. “Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina, na hatuijui kesho yake,” alisema Rais Dkt. Samia.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeendelea kutekeleza ahadi za Mhe. Samia Suluhu Hassan la utoaji ufadhili wa masomo kwa wanasayansi kupitia “Samia Scholarship” ili kuongeza wigo wa wanasayansi nchini ikiwemo sayansi ya Data na Akili unde. Prof. Mkenda amesema kuwa katika eneo hilo vijana 50 wanaenda katika vyuo vikuu bora nje ya nchi. Kati yao vijana 16 wanaondoka tarehe 1 Februari kwenda Chuo Kikuu cha Johannesburg kusomea shahada ya kwanza katika sayansi ya data na akili unde na Vijana wengine 34 wanatarajiwa kwenda Ireland mwezi Machi. Amesema vyuo wanavyo kwenda kusoma pamoja na kuwa kuwa vina mfumo mzuri wa kupeleka vijana katika makampuni makubwa katika nchi hizo kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo.

Dodoma. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa wito kwa Watanzania wote kushiriki katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kufikia lengo kuu la kujenga Taifa jumuishi, lenye ustawi, la haki na linalojitegemea. Rais Dkt. Samia aliyasema hayo Alhamis, Julai 17, 2025, katika hafla ya uzinduzi wa Dira uliofanyika jijini Dodoma katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete (JKCC)—tukio ambalo pamoja na viongozi wengine lilihudhuriwa na Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu. Aidha, Rais Dkt. Samia alisema Dira 2050 ni matokeo ya mchakato jumuishi uliohusisha maoni ya wananchi na wadau wote na inalenga kufanikisha maendeleo jumuishi kwa kizazi cha sasa na kijacho. Rais Dkt. Samia alisema Dira hiyo iliyozingatia matarajio ya Watanzania imejengwa juu ya msingi wa mafanikio na mafunzo ya historia ya maendeleo ya Tanzania tangu Uhuru, ikiwa ni pamoja na mafanikio na changamoto ya utekelezaji wa Dira ya 2025. “Maudhui ya Dira 2050 yametokana na maoni na matakwa ya Watanzania wenyewe. Tumefikiri wenyewe, tumeandika wenyewe, tumepanga wenyewe na tutatekeleza wenyewe,” alisema Mhe. Rais. Rais Dkt. Samia alisema kuwa uandaaji wa Dira hii umezingatia muktadha wa sasa wa dunia unaogusa masuala muhimu kama vile mabadiliko ya mfumo wa uchumi wa dunia, mabadiliko ya tabianchi, ongezeko kubwa la vijana nchini na mapinduzi ya kiteknolojia. Aliongeza kuwa kwa ukubwa wa rasilimali, ari na uwezo wa wananchi, Tanzania ina kila sababu ya kuweka na kufikia malengo makubwa ya maendeleo iliyojiwekea, ikiwa ni pamoja na lengo kuu la kuwa nchi ya kipato cha kati cha juu yenye uchumi wa $1 trilioni ifikapo mwaka 2050. alisema kuwa uandaaji wa Dira hii umezingatia muktadha wa sasa wa dunia unaogusa masuala muhimu kama vile mabadiliko ya mfumo wa uchumi wa dunia, mabadiliko ya tabianchi, ongezeko kubwa la vijana nchini na mapinduzi ya kiteknolojia. Aliongeza kuwa kwa ukubwa wa rasilimali, ari na uwezo wa wananchi, Tanzania ina kila sababu ya kuweka na kufikia malengo makubwa ya maendeleo iliyojiwekea, ikiwa ni pamoja na lengo kuu la kuwa nchi ya kipato cha kati cha juu yenye uchumi wa $1 trilioni ifikapo mwaka 2050.

© 2026 Idara ya Habari-MAELEZO. 

Get the App

Get it on

Microsoft Store

Available on the

App Store