Karibu!

Tunakukaribisha kwenye tovuti rasmi ya Msemaji Mkuu wa Serikali upate taarifa na habari sahihi zenye kuakisi malengo ya Serikali, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na matarajio ya Watanzania.

Mawasiliano

Tufuatilie

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) imetoa rai kwa Watanzania, taasisi za umma na binafsi pamoja na wadau wa maendeleo kuunga mkono harambee maalumu ya kuchangia matibabu ya upandikizaji figo na uloto kwa wagonjwa wenye uhitaji, hususan watoto wenye ugonjwa wa selimundu. Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali hiyo, Prof Abel Makubi amesema harambee hiyo ni sehemu ya kilele cha maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwa hospitali hiyo mwaka 2015, ambapo lengo ni kukusanya shilingi bilioni saba ndani ya kipindi cha miaka miwili ili kusaidia kuwatibu wananchi wasioweza kumudu gharama za matibabu hayo. Amesema hospitali hiyo imeendelea kukua na kuwa kituo kikubwa cha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi nchini, ikiwa na wataalamu wa afya zaidi ya 100 na kutoa huduma 20 za ubingwa pamoja na huduma 18 za ubingwa bobezi. Baadhi ya huduma zinazotolewa ni upasuaji wa moyo, upandikizaji figo, upandikizaji uloto, upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu, pamoja na huduma nyingine za kisasa zinazopatikana ndani ya nchi. “Tangu kuanza kwa huduma za upandikizaji figo mwaka 2018, jumla ya wagonjwa 56 wamefanyiwa upandikizaji wa figo nchini hatua iliyookoa zaidi ya shilingi bilioni 1.7 ambazo zingetumika kama wagonjwa hao wangetibiwa nje ya nchi”, amesema Prof. Makubi. “Vile vile huduma za upandikizaji uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu zilianza mwaka 2023 ambapo hadi sasa watoto 30 wamefanyiwa upandikizaji huo kwa mafanikio ikiwemo mtoto mmoja kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambapo huduma hizo zimeokoa zaidi ya shilingi bilioni 1.3 ambazo zingetumika kwa matibabu nje ya Tanzania”, amemalizia Prof. Makubi. Prof. Makubi ameongeza kuwa licha ya mafanikio hayo, gharama za matibabu ya upandikizaji figo na uloto bado ni kubwa kwa wananchi wengi jambo lililoifanya kuanzisha mfuko maalumu wa kusaidia wagonjwa wenye uhitaji kwa kushirikiana na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF). Kwa niaba ya Hospitali hiyo, Prof. Makubi ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika katika sekta ya afya hususan katika kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi hospitalini hapo.

Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Gerson Msigwa, amesema kuwa ujio wa wanamichezo wa kimataifa nchini Tanzania akiwemo mchezaji na nahodha wa zamani wa Klabu ya Manchester United na timu ya taifa ya Uingereza, Rio Ferdinand unashawishi wawekezaji kuwekeza katika sekta hiyo. Bw. Msigwa ameeleza hayo Mei 20, 2026 wakati akiwa safarini na mwanamichezo huyo kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma kwa kutumia treni ya Reli ya Kisasa (SGR) ikiwa ni siku ya pili ya ziara yake nchini. Ameongeza  kuwa wachezaji wa kimataifa wanapokuja nchini wanaongeza macho ya wadau mbalimbali wa michezo kuitazama nchi ya Tanzania na kuona ni namna gani wataweza kuwekeza  na nchi itaweza kunufaika kwa kupata mitaji ya kuwekeza kwenye michezo, wataalam wa kushirikiana nao pamoja na kutengeneza fursa kwa vijana kunufaika na fursa ziliozopo duniani kupitia sekta hiyo. “Ujio wa mwanamichezo huyu, unapeleka ujumbe duniani kwamba Tanzania imejidhatiti kufanya mambo makubwa kwenye sekta ya michezo hivyo kupitia wao, nchi itafanikiwa kushawishi uwekezaji katika sekta ya michezo kwani nchi yetu ina changamoto kubwa kwenye eneo la uwekezaji hasa kwenye miundombinu ya michezo pamoja na vifaa vya michezo ikiwemo jezi za wachezaji, viatu, mipira ambavyo tunaagiza kutoka nje. Vile vile, tunahitaji wataalam wa michezo ambao wataleta ujuzi wa namna ya kutengeneza viwanja.” Amesema Msigwa. Kwa upande wake, Mchezaji na Nahodha wa zamani wa Klabu ya Manchester United na timu ya taifa ya Uingereza, Rio Ferdinand amesema kuwa mpira wa miguu ukitumika vizuri unaweza kufungua fursa mbalimbali pamoja na maendeleo ya kijamii na kiuchumi.  Amesema kuwa anaendelea kufanya mazungumzo na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda pamoja na wadau wa sekta ya utalii ili kuongeza hamasa na ufuatiliaji wa sekta hiyo.