Karibu!

Tunakukaribisha kwenye tovuti rasmi ya Msemaji Mkuu wa Serikali upate taarifa na habari sahihi zenye kuakisi malengo ya Serikali, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na matarajio ya Watanzania.

Mawasiliano

Tufuatilie

Blogu

Na Baraka Messa – MAELEZO Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) imeendelea kujidhihirisha kuwa kitovu cha huduma za matibabu ya kibingwa na kibingwa bobezi nchini Tanzania na Afrika Mashariki, kufuatia uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika kipindi cha miaka 10 uliowezesha hospitali hiyo kutoa huduma ambazo hazipatikani katika hospitali nyingi za ukanda huu. Hayo yanaelezwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni kuhusu mafanikio ya uwekezaji uliofanywa na Serikali katika sekta ya afya. Msigwa anasema Serikali imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 283 kuimarisha Hospitali ya Benjamin Mkapa ili ifikie viwango vya kimataifa katika utoaji wa huduma za matibabu ya kibingwa. “Hospitali ya Benjamin Mkapa leo inatoa huduma ambazo hazipatikani katika hospitali nyingine nyingi si Tanzania pekee, bali hata katika Afrika Mashariki, Serikali imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 283 katika kipindi cha miaka 10 kuifanya hospitali hii kuwa kituo cha kisasa cha matibabu ya kibingwa na kibingwa bobezi,” anasema Msigwa. Anafafanua kuwa uwekezaji huo umehusisha ujenzi wa majengo ya kisasa ya kutolea huduma za kibingwa, ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa vinavyokidhi viwango vya kimataifa, uboreshaji wa mifumo ya Tehama pamoja na kuongeza idadi ya wataalamu wa afya na kuboresha mazingira yao ya kazi. Msigwa anasema mwaka 2015 hospitali hiyo ilikuwa na watumishi 20 pekee, lakini kufikia mwaka 2026 idadi hiyo imeongezeka na kufikia watumishi 1,076, wakiwemo madaktari bingwa 105. Anasema hospitali hiyo sasa inatoa huduma 17 za kibingwa bobezi, zikiwemo upandikizaji wa figo, upandikizaji wa uloto kwa wagonjwa wa seli mundu, upasuaji wa moyo kwa kufungua kifua, uchunguzi wa mishipa ya moyo, upasuaji wa ubongo na uti wa mgongo, ubadilishaji wa nyonga na magoti, huduma za radiolojia ya kisasa pamoja na uchujaji wa damu (dialysis). “Huduma za upandikizaji wa uloto kwa wagonjwa wa seli mundu zinapatikana Hospitali ya Benjamin Mkapa na ni miongoni mwa huduma adimu ambazo hazipatikani katika hospitali nyingine nyingi nchini na Afrika Mashariki,” anaeleza . Msigwa anasema kuimarika kwa huduma hizo kumepunguza kwa kiwango kikubwa idadi ya Watanzania waliokuwa wakisafiri nje ya nchi kutafuta matibabu, jambo ambalo limeokoa fedha nyingi za Serikali na wananchi. HOSPITALI BENJAMINI YAWA KIVUTIO WAGONJWA KUTOKA MATAIFA YA NJE Msigwa anasema hospitali hiyo sasa imekuwa kivutio cha wagonjwa kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika. “Tumewahudumia wagonjwa 2,897 kutoka Burundi na wagonjwa 526 kutoka Comoro. Pia wagonjwa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na nchi nyingine za Afrika Mashariki wanaendelea kuja kupata matibabu hapa, Tunawatibu ndugu zetu, lakini pia huu ni utalii wa matibabu unaoingizia taifa mapato,” anasema Msigwa. Anasema kuwa mafanikio hayo yanaifanya Tanzania kuanza kushindana na mataifa yaliyopiga hatua katika utalii wa matibabu kama India, ambayo kwa miaka mingi yamekuwa yakipokea wagonjwa wengi kutoka Tanzania. “Kwa muda mrefu Watanzania walikuwa wakitumia fedha nyingi kwenda kutibiwa nje ya nchi, hususan India,..Sasa Serikali imewekeza kuhakikisha huduma hizo zinapatikana hapa nchini ili wananchi wapate matibabu bora na wakati huohuo Tanzania inufaike kupitia utalii wa matibabu,” anasema Msigwa. Pia Msigwa amesema Julai 10, 2025 Hospitali ya Benjamin Mkapa ilianzisha International Clinic, kitengo maalumu kinachotoa huduma kwa wagonjwa wa ndani na wa kimataifa. Anasema tangu kuanzishwa kwa huduma hiyo, wagonjwa 18,607 wamehudumiwa, wakiwemo wagonjwa 390 kutoka mataifa mbalimbali, huku huduma ya Master Health Check-up ikiendelea kuvutia watu wanaohitaji uchunguzi wa afya kwa kiwango cha kimataifa. Aidha anasema hospitali hiyo pia imeanzisha eneo maalumu la huduma binafsi kwa wagonjwa wanaohitaji faragha na huduma za kiwango cha juu bila kuchangamana na wagonjwa wengine. Anasema Huduma hizi zinafanana na zile zinazotolewa katika hospitali za kisasa duniani kama za China, Ujerumani na India, huku dhamira ya Serikali ikiwa ni kuhakikisha Watanzania wanapata huduma bora ndani ya nchi na wakati huohuo Tanzania inakuwa kitovu cha utalii wa matibabu barani Afrika. Kuimarika kwa Hospitali ya Benjamin Mkapa na hospitali mbalimbali za rufaa nchini ni sehemu ya malengi ya Serikali ya kuboresha sekta ya afya, kuongeza upatikanaji wa huduma za kibingwa na kuiweka Tanzania katika nafasi ya ushindani wa kimataifa katika utoaji wa huduma za matibabu.

Na Josephina Lupasha na Immaculate Makilika – MAELEZO Ulimwenguni kote miundombinu imeendelea kuwa msingi wa ukuaji wa uchumi. Barabara, reli, bandari, viwanja vya ndege, nishati na teknolojia ya mawasiliano ni muhimu katika kupunguza gharama za uzalishaji na usafirishaji, kuunganisha masoko na kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa. Kwa upande wa Afrika, kupitia taasisi ya fedha Africa50 inayoshirikiana na Serikali mbalimbali barani Afrika inabadili taswira na hadhi ya Afrika kwa kusaidia ujenzi wa miundombinu ya kimkakati, uwekezaji wenye tija na mageuzi ya kiuchumi na teknolojia barani humo. Taasisi hiyo inaandaa miradi hadi kufikia hatua ya kupata wawekezaji na kutafuta wawekezaji kwa utaratibu wa equity investment kupitia ubia kati ya Serikali na sekta binafsi kutoka kwa wawekezaji na wafadhili wa ndani na nje ya Afrika. Lengo ni kuharakisha utekelezaji wa miundombinu yenye ubora kwa kuzingatia thamani ya fedha. Aidha, miundombinu ya kipaumbele ni pamoja na nishati, uchukuzi, elimu, afya, mawasiliano na fedha (fintech). Ili kuendelea kutoa mchango wake hadhimu kwa Afrika, Tanzania imeendelea kujijengea nafasi muhimu katika ramani ya uwekezaji na maendeleo ya miundombinu barani Afrika kwa kuamua kuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Africa50 (Africa50 General Shareholders’ Meeting – GSM) na Jukwaa la Miundombinu Afrika (Infra for Africa Forum), lililofanyika Agosti 5 – 6, 2026, jijini Dar es Salaam. Hivyo inategemewa mkutano utavutia wawekezaji wa kimataifa kutangaza miradi ya kimkakati kama reli ya SGR, Bandari ya Dar es Salaam, uzalishaji wa umeme, na miundombinu ya TEHAMA. Mkutano huo ambao umeleta pamoja viongozi wa Serikali, taasisi za fedha za kimataifa, wanahisa wa Africa50, wawekezaji, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kutoka ndani na nje ya Afrika, katika jitihada za kutafuta namna ya kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati inayolenga kuleta mageuzi ya kiuchumi barani Afrika, umekuwa nyenzo muhimu ya kuutangazia ulimwengu kuhusu utayari wa Afrika na kutumia fursa zake Afrika katika kujiletea maendeleo ya kweli. Kwa Tanzania, mkutano huo umekuwa zaidi ya tukio la kimataifa, umekuwa fursa ya kuonesha uwezo, fursa na mwelekeo wa nchi katika kujenga uchumi unaotegemea miundombinu ya kisasa, uwekezaji, ubunifu na ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi. Akizungumza katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, anasema kuwa kuongezeka kwa imani kwa Tanzania kunatokana na mabadiliko ya kiuchumi yanayoendelea nchini, fursa za uwekezaji na nafasi yake ya kimkakati kama lango linalounganisha Afrika na masoko ya kimataifa. Aidha, anasema Afrika inapaswa kujenga mustakabali wake kupitia uongozi madhubuti, mitaji na ushirikiano wa waafrika wenyewe, na kuwa bara la Afrika linaweza kutumia rasilimali zake, mitaji ya ndani na fursa zilizopo ili kupunguza pengo la maendeleo, kuongeza biashara na kuimarisha ushindani wake katika uchumi wa dunia. “Wananchi hawapimi maendeleo kwa matamko, bali kwa matokeo wanayoyaona katika maisha yao, Kwa msingi huo, Serikali na wadau wa maendeleo wanapaswa kuhakikisha wananchi wanapata barabara bora, nishati ya uhakika, bandari zenye ufanisi, reli za kisasa, miundombinu ya kidijitali na huduma nyingine zinazochochea uzalishaji, ajira na biashara” anasema Rais Samia. Akionesha utayari wa hatua iliyopigwa na Tanzania katika kuleta mageuzi ya kiuchumi anasema tayari imeweka msingi kupitia miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo upanuzi na uboreshaji wa Bandari ya Dar es Salaam, ujenzi wa reli ya kisasa (SGR), ujenzi na uboreshaji wa barabara na madaraja, maendeleo ya viwanja vya ndege pamoja na miradi ya nishati na miundombinu ya TEHAMA. Hata hivyo katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo Tanzania 2050, yanayolenga kujenga uchumi shindani, jumuishi na unaotegemea viwanda, ubunifu, rasilimali watu, maendeleo endelevu na miundombinu ya kisasa. Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa sekta binafsi kuwa mhimili wa ukuaji wa uchumi, huku ikilenga kuweka mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji kwa kuwa na miundombinu ya kimkakati na kujenga ubia unaoweza kuvutia mitaji binafsi, teknolojia na ubunifu. Kwa hakika, Tanzania inaendelea kubaki na nafasi muhimu kama lango la nchi zisizo na bandari katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati pia inatoa fursa kubwa ya kuifanya nchi kuwa kitovu cha usafirishaji, biashara na uwekezaji. Uwezo wa bandari, reli, barabara na nishati unapoimarishwa kwa pamoja, Tanzania inaweza kuongeza mchango wake katika minyororo ya thamani ya kikanda na bara. Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Dkt. Sidi Quld Tah akizungumza pia katika Mkutano huo wa Africa50 anasema kuwa Afrika inapaswa kutumia rasilimali zake, ikiwemo gesi asilia, kwa ufanisi ili kuchochea ukuaji wa viwanda, kuimarisha ustahimilivu wa nishati na kuboresha maisha ya wananchi. Anasisitiza “Akiba ya gesi asillia barani Afrika inafikia takribani asilimia saba ya akiba ya gesi duniani, rasilimali hizi zikitumika kwa busara zinaweza kusaidia kuimarisha viwanda, kuongeza ustahimilivu wa nishati na kuchochea ustawi wa wananchi wetu”. Dkt. Tah anapendekeza kuwa ili Afrika itimize malengo yake na kupata maendeleo inayokusudia inatakiwa kufanyika kwa uwekezaji wa haraka barani humo, kuimarisha matumizi ya mitaji ya ndani, mifumo ya kifedha na taasisi za kifedha ili kuziba pengo la ufadhili wa miundombinu. Aidha, anaeleza kuwa Afrika kwa kushirikiana Benki ya Maendeleo ya Afrika pamoja na Afrika50 zitaendelea kutekeleza jukumu muhimu katika kuandaa miradi inayoweza kufadhiliwa, kupunguza hatari za uwekezaji na kuvutia mitaji zaidi. Naye, Waziri wa Fedha wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, anasema kuwa uamuzi huo wa Africa50 kwa kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa Infra for Africa Forum, ni heshima na ishara ya imani kwa Tanzania pamoja na maono yake ya kujenga Afrika iliyounganishwa, yenye ustawi na maendeleo. “Kwa kipindi cha miaka 10, Africa50 imejijenga kama taasisi muhimu katika kuchochea uwekezaji wa miundombinu barani Afrika kupitia uandaaji wa miradi, uhamasishaji wa mitaji na uwekezaji wa kimkakati,” anasema Balozi Omar Tanzania, imekuwa mwananchama katika Africa50 kuanzia mwaka 2023, ambao umefungua fursa ya nchi kushiriki katika mfumo mpana wa kuandaa miradi, kuhamasisha uwekezaji na kukuza maendeleo endelevu ya miundombinu. Balozi Omar anaeleza manufaa ya uanachama wa Tanzania katika Taasisi hiyo kuwa ni pamoja na kuhusisha maandalizi na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati nchini, ikiwemo maendeleo ya Bandari ya Mangapwani Zanzibar, Mradi wa Mini LNG, miundombinu ya usafirishaji wa umeme pamoja na ushirikiano katika upanuzi wa huduma za usafishaji wa figo kupitia ubia kati ya sekta ya umma na binafsi. Inaelezwa kuwa kupitia Mkutano huo pia umeiwezesha Tanzania kuwasilisha fursa mbalimbali

▪️Ujenzi Wake Kuanza Oktoba 2026 ▪️Fidia Shilingi bil 8.5 Imeshalipwa kwa Wananchi Waliopisha Mradi Na Adelina Johnbosco – MAELEZO Tatizo la uhaba wa maji katika baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Dodoma linaelekea kupata ufumbuzi wa kudumu kufuatia ujenzi wa Mradi wa Bwawa la Farkwa utakaoanza kujengwa Oktoba mwaka huu. Bwawa hilo litakalojengwa wilayani Chemba, kata ya Farkwa mkoani Dodoma litakuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni 128 kwa siku na kuhifadhi lita bilioni 390 na linatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 22. Bwawa hili litahudumia hasa wilaya za Chemba, Bahi, Chamwino na maeneo mengine ndani na maeneo ya karibu na mkoa wa Dodoma, lengo ni kutokomeza kabisa upungufu wa maji ndani ya mkoa huo. Ujenzi wa bwawa la Farkwa utatekelezwa na Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa gharama ya Shilingi bilioni 163.43 hadi kukamilika kwake. Aidha, jumla ya Shilingi bilioni 8.5 zimelipwa kama fidia kwa wananchi kutoka katika vijiji viwili vya Mombose na Bubutole waliopisha ujenzi. “Tuliambiwa tunahamishwa na kulipwa, mwaka 2017 tathmini ilifanyika katika maeneo yetu, ila ukiwa bado hujapokea kitu mkononi unaona kama haiwezekani, lakini mwaka 2019 tukalipwa fidia zetu, tukaanza maisha mapya na yenye matumaini zaidi katika kijiji cha Sankwaleto kwenye makazi mapya” Bi. Rahma Petro, mkazi wa Farkwa Hadi hapa, tayari inaonekana Dodoma yenye ukijani wakati wote, iwe mvua iwe jua, hakuna tena ukame katika mkoa huu pale mradi huu utakapokuwa umekamilika, yale yaliyokuwa yanasubiriwa kufanyika wakati wa kipindi cha mvua pekee yatafanyika pia kipindi cha kiangazi. “Tumeajiandaa kwa vingi kwa kweli, kijamii na kiuchumi, tutalima kilimo cha umwagiliaji, tutafuga samaki na mengine mengi, ni furaha tupu. Hii ilikuwa ni hadithi ya muda mrefu ambayo tumezaliwa tukaikuta kutoka kwa wazee wetu, hakika leo inatimia” Bw. Suleiman Gawa, mkazi wa Farkwa Akiwa katika eneo utakapotekelezwa mradi huo, hivi karibuni, Bw. David Manyama, Mhaidrojiolojia ambaye ni mtaalam wa maji chini ya ardhi kutoka Wizara ya Maji, amebainisha uwepo wa maji ya akiba kwa watumiaji kutokana na wingi wa lita za maji utaokaozalishwa na bwawa hilo. “Mradi huu unaanza mwezi Oktoba, 2026, maandalizi yako tayari na baada ya kukamilika kwa mradi, si kwamba utaondoa kero ya maji tu bali hata kuchochea miradi mbali mbali ya kiuchumi kama vile kilimo cha umwagiliaji kisichosubiri msimu, ufugaji wa samaki na itakuwa ongezeko la maji katika hifadhi ya pori la akiba Swagaswaga Chemba, wanyama hifadhini watapata maji ya kunywa ya kutosha tofauti na hali ilivyo kwa sasa” Bw. David Manyama, Mhaidrojiolojia Mradi huu mwisho wake ni kuleta maji, lakini suala la ajira wakati na baada ya mradi ni vitu vinavotegemewa pakubwa. Mwenyekiti wa kijiji chenye makazi mapya cha Sankwaleto, akaongea kuhusu wazawa kupata fursa mbalimbali kutokana na mradi huo. “Kama kiongozi tumeshashirikishwa na kuhakikishiwa kwamba, sisi wazawa tutapewa kipaumbele katika fursa mbalimbali zinazotokana na huu mradi ikiwemo ajira wakati na baada ya ujenzi, hivyo nawasihi vijana na wakazi wenzangu wa hapa kuwa tayari, tusikubali kukaa kinyonge katika kuchangamkia fursa katika hizi” Bw. Khalifa Salum, mwenyekiti wa kijiji chenye makazi mapya Sankwaleto Si nyumba na umiliki wa ardhi pekee kwenye maeneo ya makazi mapya waliohamia wananchi waliopisha mradi, bali shule na zahanati vimejengwa kwa ajili ya kuwahudumia. “Kijiji cha Sankwaleto kimejengwa shule ya msingi na imeshaanza kazi, kuna nyumba za walimu na wanafunzi wote waliokuwa wakisoma kule kwenye vijiji vya zamani wako kwenye shule mpya wanaendelea na masomo, hakuna kilichosimama, pia zahanati inayowahudumia wananchi, kwa kweli tunashukuru sana” – Bi. Agnes Msote, Diwani wa kata ya Farkwa Kukamilika kwa Bwawa la Farkwa kunatarajiwa kuimarisha usalama wa maji katika jiji la Dodoma na kuchangia kwa kiasi kikubwa maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi katika mkoa huo. Juhudi hizo zinaendana na azma ya Serikali ya kuimarisha upatikanaji wa huduma za maji nchini kwa kuzingatia usimamizi endelevu wa rasilimali za maji na upatikanaji wake maeneo yote hasa katika maeneo ya vijijini pamoja na kuhakikisha juhudi za kufikisha huduma za maji katika vijiji vyote nchini linatimia ili kumtua mwanamke ndoo kichwani.