Na Bupe Mwaiseje – MAELEZO Mageuzi ya kidijitali katika sekta ya ununuzi wa umma yanaendelea kuleta matokeo makubwa nchini kupitia mfumo wa Kitaifa wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST) ambao umekua mkombozi kwa watoa huduma na Serikali, ukiimarisha uwazi, uwajibikaji na ushindani katika matumizi ya fedha za umma. Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) Bw. Dennis Simba anabainisha hayo katika Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma lililowakutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali kujadili namna teknolojia inavyoweza kuongeza ufanisi wa ununuzi wa umma na kuharakisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Kongamano hilo lililofanyika jijini Arusha lililoogozwa na kaulimbiu isemayo “Kutumia Fursa ya Ununuzi wa Umma Kidijitali Kufikia Uchumi Endelevu, Jumuishi na Shindani kuelekea Dira ya Taifa 2050,” limeonesha kuwa ununuzi wa umma si shughuli ya kiutawala pekee, bali ni nyenzo muhimu ya kuchochea ukuaji wa uchumi, kuongeza ushindani wa biashara na kuhakikisha rasilimali za umma zinatumika kwa tija. Mkurugenzi huyo wa PPRA anaeleza kuwa tangu kuanza kutumika rasmi kwa mfumo huo, Julai 1, 2023, uendeshaji wa shughuli za ununuzi nchini kwa kiasi kikubwa umebadilika kwa kuwa mfumo huo unawezesha usajili wa wazabuni, uchakataji wa zabuni kwa njia ya mtandao, usimamizi wa mikataba, malipo ya mikataba, minada ya kielektroniki pamoja na matumizi ya katalogi ya bidhaa na huduma. Mbali na kurahisisha utoaji wa huduma, Bw. Simba anasema PPRA imeendelea kuuboresha mfumo huo kwa kuanzisha moduli ya kisasa ya ufuatiliaji wa vihatarishi katika michakato ya ununuzi kwa wakati halisi. Teknolojia hiyo inaiwezesha Mamlaka kubaini mapema viashiria vinavyoweza kusababisha upotevu wa fedha za umma au kukiukwa kwa taratibu za ununuzi, ikiwemo upangaji wa matokeo ya zabuni, ushindani usioridhisha, kula njama kati ya wazabuni na vitendo vya udanganyifu. Anasema hatua hiyo imeongeza uwezo wa PPRA kuchukua hatua za haraka kabla dosari hazijasababisha hasara kwa Serikali, huku ikiimarisha uadilifu na uwazi katika mnyororo mzima wa ununuzi wa umma. Mafanikio ya matumizi ya NeST yameonekana kupitia ongezeko la ushiriki wa wadau ambapo hadi Juni 30, 2026, zaidi ya wazabuni 45,270 walikuwa wamesajiliwa katika mfumo huo, huku asilimia 95 wakiwa wazabuni wa ndani. Aidha, zaidi ya taasisi nunuzi 62,847 na watumiaji zaidi ya 161,704 walikuwa wakitumia mfumo huo. Anasema katika kipindi hicho, zabuni 286,903 zilitangazwa kupitia NeST na zaidi ya tuzo za zabuni 181,057 zenye thamani ya shilingi trilioni 14.5 zikatolewa kwa njia ya mfumo huo, hatua inayoonesha kuongezeka kwa matumizi ya teknolojia katika kusimamia fedha za umma. Aidha, ameeleza kuwa PPRA imeendelea kuwezesha ushiriki wa makundi maalumu katika fursa za zabuni. Kupitia utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023, Taasisi Nunuzi zinatakiwa kutenga asilimia 30 ya bajeti ya ununuzi kwa ajili ya vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu. Matokeo ya utekelezaji huo yanaonekana ambapo hadi Julai 28, 2026 zaidi ya makundi maalumu 23,590 yalikuwa yamesajiliwa katika NeST na tuzo 745 zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 53.68 zilitolewa kwa makundi maalumu. Hii inaonesha kuwa mageuzi ya kidijitali hayajaboresha tu ufanisi wa Serikali, bali pia yamepanua fursa za kiuchumi kwa makundi yaliyokuwa hayashiriki kwa kiwango kikubwa hapo awali. Mbali na manufaa ya kiuchumi, matumizi ya NeST yamechangia pia utunzaji wa mazingira. Utafiti wa PPRA unaonesha kuwa matumizi ya mfumo huo yalipunguza uzalishaji wa metariki tani 64,028 za hewa ya ukaa katika mwaka wa fedha 2023/2024 kutokana na kupungua kwa matumizi ya karatasi. Mafanikio hayo yameifanya Tanzania kutambulika kimataifa. Mfumo wa NeST umepata tuzo mbalimbali za ubunifu na mazingira, ikiwemo kutajwa miongoni mwa mifumo 20 bora ya Serikali duniani katika tuzo za World Summit on the Information Society (WSIS) Prizes 2026 zilizofanyika Geneva, Uswizi. Sambamba na mafanikio hayo, PPRA imeendelea kuimarisha ukaguzi wa ukidhi na thamani halisi ya fedha ili kuhakikisha taasisi zote zinazingatia sheria na taratibu za ununuzi wa umma. Jitihada hizo zinaenda sambamba na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuongeza uwajibikaji, kudhibiti mianya ya ubadhirifu na kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa manufaa ya wananchi. Kadhalika, Mamlaka hiyo imeendelea kupanua ushirikiano na taasisi za ndani na nje ya nchi kupitia kubadilishana uzoefu katika ununuzi endelevu, huku nchi mbalimbali za Afrika pamoja na Benki ya Dunia zikiendelea kuja kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa kujenga na kutumia Mfumo wa NeST. Kwa ujumla, mafanikio ya PPRA yanaonesha kuwa uwekezaji katika mifumo ya kidijitali si tu umeongeza uwazi na ufanisi wa ununuzi wa umma, bali pia umeifanya sekta hiyo kuwa chombo muhimu cha kukuza uchumi shindani, jumuishi na endelevu. Kadiri matumizi ya NeST yanavyoendelea kuongezeka, ndivyo nafasi ya ununuzi wa umma katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inavyozidi kuimarika.