Karibu!

Tunakukaribisha kwenye tovuti rasmi ya Msemaji Mkuu wa Serikali upate taarifa na habari sahihi zenye kuakisi malengo ya Serikali, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na matarajio ya Watanzania.

Mawasiliano

Tufuatilie

Na Bupe Mwaiseje – MAELEZO Mageuzi ya kidijitali katika sekta ya ununuzi wa umma yanaendelea kuleta matokeo makubwa nchini kupitia mfumo wa Kitaifa wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST) ambao umekua mkombozi kwa watoa huduma na Serikali, ukiimarisha uwazi, uwajibikaji na ushindani katika matumizi ya fedha za umma. Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) Bw. Dennis Simba anabainisha hayo katika Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma lililowakutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali kujadili namna teknolojia inavyoweza kuongeza ufanisi wa ununuzi wa umma na kuharakisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Kongamano hilo lililofanyika jijini Arusha lililoogozwa na kaulimbiu isemayo “Kutumia Fursa ya Ununuzi wa Umma Kidijitali Kufikia Uchumi Endelevu, Jumuishi na Shindani kuelekea Dira ya Taifa 2050,” limeonesha kuwa ununuzi wa umma si shughuli ya kiutawala pekee, bali ni nyenzo muhimu ya kuchochea ukuaji wa uchumi, kuongeza ushindani wa biashara na kuhakikisha rasilimali za umma zinatumika kwa tija. Mkurugenzi huyo wa PPRA anaeleza kuwa tangu kuanza kutumika rasmi kwa mfumo huo, Julai 1, 2023, uendeshaji wa shughuli za ununuzi nchini kwa kiasi kikubwa umebadilika kwa kuwa mfumo huo unawezesha usajili wa wazabuni, uchakataji wa zabuni kwa njia ya mtandao, usimamizi wa mikataba, malipo ya mikataba, minada ya kielektroniki pamoja na matumizi ya katalogi ya bidhaa na huduma. Mbali na kurahisisha utoaji wa huduma, Bw. Simba anasema PPRA imeendelea kuuboresha mfumo huo kwa kuanzisha moduli ya kisasa ya ufuatiliaji wa vihatarishi katika michakato ya ununuzi kwa wakati halisi. Teknolojia hiyo inaiwezesha Mamlaka kubaini mapema viashiria vinavyoweza kusababisha upotevu wa fedha za umma au kukiukwa kwa taratibu za ununuzi, ikiwemo upangaji wa matokeo ya zabuni, ushindani usioridhisha, kula njama kati ya wazabuni na vitendo vya udanganyifu. Anasema hatua hiyo imeongeza uwezo wa PPRA kuchukua hatua za haraka kabla dosari hazijasababisha hasara kwa Serikali, huku ikiimarisha uadilifu na uwazi katika mnyororo mzima wa ununuzi wa umma. Mafanikio ya matumizi ya NeST yameonekana kupitia ongezeko la ushiriki wa wadau ambapo hadi Juni 30, 2026, zaidi ya wazabuni 45,270 walikuwa wamesajiliwa katika mfumo huo, huku asilimia 95 wakiwa wazabuni wa ndani. Aidha, zaidi ya taasisi nunuzi 62,847 na watumiaji zaidi ya 161,704 walikuwa wakitumia mfumo huo. Anasema katika kipindi hicho, zabuni 286,903 zilitangazwa kupitia NeST na zaidi ya tuzo za zabuni 181,057 zenye thamani ya shilingi trilioni 14.5 zikatolewa kwa njia ya mfumo huo, hatua inayoonesha kuongezeka kwa matumizi ya teknolojia katika kusimamia fedha za umma. Aidha, ameeleza kuwa PPRA imeendelea kuwezesha ushiriki wa makundi maalumu katika fursa za zabuni. Kupitia utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023, Taasisi Nunuzi zinatakiwa kutenga asilimia 30 ya bajeti ya ununuzi kwa ajili ya vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu. Matokeo ya utekelezaji huo yanaonekana ambapo hadi Julai 28, 2026 zaidi ya makundi maalumu 23,590 yalikuwa yamesajiliwa katika NeST na tuzo 745 zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 53.68 zilitolewa kwa makundi maalumu. Hii inaonesha kuwa mageuzi ya kidijitali hayajaboresha tu ufanisi wa Serikali, bali pia yamepanua fursa za kiuchumi kwa makundi yaliyokuwa hayashiriki kwa kiwango kikubwa hapo awali. Mbali na manufaa ya kiuchumi, matumizi ya NeST yamechangia pia utunzaji wa mazingira. Utafiti wa PPRA unaonesha kuwa matumizi ya mfumo huo yalipunguza uzalishaji wa metariki tani 64,028 za hewa ya ukaa katika mwaka wa fedha 2023/2024 kutokana na kupungua kwa matumizi ya karatasi. Mafanikio hayo yameifanya Tanzania kutambulika kimataifa. Mfumo wa NeST umepata tuzo mbalimbali za ubunifu na mazingira, ikiwemo kutajwa miongoni mwa mifumo 20 bora ya Serikali duniani katika tuzo za World Summit on the Information Society (WSIS) Prizes 2026 zilizofanyika Geneva, Uswizi. Sambamba na mafanikio hayo, PPRA imeendelea kuimarisha ukaguzi wa ukidhi na thamani halisi ya fedha ili kuhakikisha taasisi zote zinazingatia sheria na taratibu za ununuzi wa umma. Jitihada hizo zinaenda sambamba na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuongeza uwajibikaji, kudhibiti mianya ya ubadhirifu na kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa manufaa ya wananchi. Kadhalika, Mamlaka hiyo imeendelea kupanua ushirikiano na taasisi za ndani na nje ya nchi kupitia kubadilishana uzoefu katika ununuzi endelevu, huku nchi mbalimbali za Afrika pamoja na Benki ya Dunia zikiendelea kuja kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa kujenga na kutumia Mfumo wa NeST. Kwa ujumla, mafanikio ya PPRA yanaonesha kuwa uwekezaji katika mifumo ya kidijitali si tu umeongeza uwazi na ufanisi wa ununuzi wa umma, bali pia umeifanya sekta hiyo kuwa chombo muhimu cha kukuza uchumi shindani, jumuishi na endelevu. Kadiri matumizi ya NeST yanavyoendelea kuongezeka, ndivyo nafasi ya ununuzi wa umma katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inavyozidi kuimarika.

Na Scolastica Sambi – MAELEZO Mkoa wa Kigoma umekuwa na nafasi ya kimkakati katika biashara ya kikanda kutokana na mwambao wake katika Ziwa Tanganyika na ukaribu wake na Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Zambia. Hata hivyo, changamoto za miundombinu ya usafirishaji zimekuwa zikizuia mkoa huo kutumia kikamilifu fursa hiyo, huku gharama za usafirishaji zikiwa kubwa na safari za mizigo kuchukua muda mrefu. Sasa hali hiyo imeanza kubadilika kupitia utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali, ikiwemo ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora–Kigoma, uzinduzi wa meli nne mpya za mizigo katika Ziwa Tanganyika pamoja na maboresho ya Bandari ya Kigoma. Miradi hiyo inatarajiwa kuibadili Kigoma kuwa kitovu muhimu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, huku ikiimarisha nafasi ya Tanzania kama lango la biashara kwa nchi zisizo na bandari. Katika kuonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha sekta ya uchukuzi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amezindua meli nne mpya za mizigo, akaweka jiwe la msingi la ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) Tabora–Kigoma na kukagua maendeleo ya maboresho ya Bandari ya Kigoma. Hatua hizo zinaakisi mkakati wa Serikali wa kuwekeza katika miundombinu ya kisasa ili kuchochea ukuaji wa uchumi na biashara. Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, anasema Kigoma itaendelea kuwa lango kuu la biashara kuelekea Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Zambia kutokana na nafasi yake ya kipekee katika Ziwa Tanganyika. Anasema kukamilika kwa Reli ya Kisasa ya Tabora–Kigoma, meli mpya za mizigo na maboresho ya Bandari ya Kigoma kutaifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha usafirishaji na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. “Kwa nafasi yake ya kipekee katika Ziwa Tanganyika, Kigoma itaendelea kuwa lango kuu la biashara kuelekea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Burundi na Zambia. Miradi hii ya SGR na meli mpya za mizigo itaifanya Tanzania kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati,” anasema Prof. Mbarawa. Meli hizo nne mpya, ambazo kila moja ina uwezo wa kubeba tani 2,000 za mizigo, zinatarajiwa kuongeza uwezo wa Bandari ya Kigoma kuhudumia zaidi ya tani 832,000 za mizigo kwa mwaka. Mbali na kuongeza ufanisi wa usafirishaji, uwekezaji huo unatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali, kuchochea biashara na kuzalisha takribani ajira 600 za moja kwa moja katika sekta mbalimbali. Kwa wakazi wa Kigoma, uwekezaji huo una maana zaidi ya kujengwa kwa miundombinu. Ni mwanzo wa zama mpya za fursa za kiuchumi, ajira na uwekezaji. Kuimarika kwa usafiri wa reli na majini kutarahisisha usafirishaji wa bidhaa, kupanua masoko na kuvutia wawekezaji ndani na nje ya nchi. Bi. Asha Mussa, mkazi wa Kibirizi, anasema wananchi wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu maendeleo ya aina hiyo. “Tunaamini meli mpya na reli ya kisasa zitafungua fursa nyingi za kiuchumi kwa wananchi. Kuimarika kwa miundombinu ya usafiri kutasaidia wafanyabiashara, vijana na wajasiriamali kupata nafasi zaidi za kujikwamua kiuchumi.” Hisia kama hizo zinaungwa mkono na wananchi wengi wanaoamini kuwa miradi hiyo itakuwa suluhisho la changamoto zilizokuwa zikiikabili sekta ya usafirishaji kwa miaka mingi. Bw. John Mwakalinga, mkazi wa Kigoma Mjini, anasema gharama kubwa za usafirishaji zimekuwa zikikwamisha biashara na kupunguza ushindani wa bidhaa katika masoko. “Kwa miaka mingi usafirishaji wa bidhaa ulikuwa na changamoto nyingi na gharama kubwa. Tunaamini SGR pamoja na maboresho ya bandari utarahisisha usafirishaji wa bidhaa kwenda masoko ya ndani na nchi jirani, kuongeza ushindani wa wafanyabiashara na kuinua kipato cha wananchi.” Mradi wa Reli ya Kisasa wa Tabora–Kigoma wenye urefu wa kilometa 506 unajengwa kwa gharama ya takribani dola za Marekani bilioni 2.7. Mradi huo utaunganisha Kigoma na mtandao wa reli ya kisasa unaofika Dar es Salaam, hivyo kuimarisha Ushoroba wa Kati kwa kurahisisha usafirishaji wa mizigo kati ya Tanzania na Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pamoja na Zambia. Faida za miradi hiyo hazitaishia katika kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo na abiria pekee. Pia zinatarajiwa kuongeza ushindani wa biashara za kikanda, kuvutia uwekezaji, kuchochea uzalishaji wa bidhaa na kuongeza mchango wa sekta ya uchukuzi katika ukuaji wa uchumi wa Taifa. Kadri miradi hiyo inavyoendelea kukamilika, Kigoma inaelekea kujidhihirisha kama kitovu kipya cha biashara katika Afrika Mashariki na Kati. Uwekezaji wa Serikali katika reli, bandari na usafiri wa majini unaweka msingi imara wa maendeleo endelevu, kuongeza fursa za ajira na kuimarisha ustawi wa wananchi. Kwa hakika, kukamilika kwa Reli ya Kisasa ya Tabora–Kigoma, kuanza kwa huduma za meli mpya za mizigo na maboresho ya Bandari ya Kigoma kutafungua ukurasa mpya wa maendeleo ya kiuchumi. Kigoma itaimarika kama lango kuu la biashara katika ukanda huu, huku Tanzania ikiendelea kujijengea nafasi kama kitovu muhimu cha usafirishaji na biashara Afrika Mashariki na Kati.