JAB Yazindua Rasmi Mwongozo wa Ithibati ya Maisha kwa Waandishi wa Habari Wakongwe
Na. Timothy Mwakyenda – MAELEZO
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Ithibati ya Maisha utakaowezesha waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango mkubwa katika maendeleo ya tasnia ya habari nchini kutambuliwa rasmi, licha ya kutokukidhi vigezo vya kielimu vilivyowekwa na Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016.
Uzinduzi wa mwongozo huo umetajwa kuwa hatua muhimu ya kutambua mchango wa wanahabari waliolitumikia taifa kwa uadilifu na weledi kwa miaka mingi kabla ya kuanza kutumika kwa masharti mapya ya kitaaluma yanayomtaka mwandishi wa habari kuwa na angalau stashahada (Diploma) ya uandishi wa habari.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya JAB, uliofanyika Julai 11, 2026 katika kijiji cha Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo katika viwanja vya Maonesho ya 50 ya kimataifa ya biashara Dar es salaam (sabasaba) Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Tildo Mhando, kupitia taarifa iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, alisema mwongozo huo unalenga kuwapa Ithibati ya Maisha waandishi wa habari wakongwe ambao wakati Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ilipopitishwa mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari.
Alieleza kuwa waandishi hao hawakupata fursa ya kusomea darasani hadi kufikia kiwango cha diploma, lakini walijijengea uwezo kupitia uzoefu na walishiriki kwa kiwango kikubwa katika maendeleo ya vyombo vya habari na ujenzi wa taifa.
“Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa kizazi cha mwanzo na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma hii” ilisisitiza taarifa hiyo.

Aidha, aliishukuru Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kushirikiana na JAB katika kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari na kusisitiza umuhimu wa weledi, uwajibikaji na maadili kwa waandishi wa habari nchini.
Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi wa JAB, Bwana Patrick Kipangula alisema kuwa uzinduzi wa Mwongozo wa Ithibati ya Maisha ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya kuhakikisha kuwa ni pamoja na kuimarisha viwango vya taaluma kupitia sheria, mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia taifa kwa uaminifu na uzalendo unaendelea kutambuliwa na kuthaminiwa.