Na. Baraka Messa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka Watanzania kuilinda na kuitunza miundombinu ya Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Julius Nyerere (JNHP), akisema kuwa mradi huo ni mali ya Watanzania na urithi muhimu kwa vizazi vya sasa na vijavyo. Rais Samia amesema hayo Agosti 22, 2026, wilayani Rufiji mkoani Pwani, wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Uzalishaji wa Umeme cha Julius Nyerere chenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115. Amesema kuwa Serikali imewekeza rasilimali kubwa katika utekelezaji wa mradi huo kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa nishati ya umeme na kuweka msingi wa maendeleo ya viwanda, uchumi na ustawi wa wananchi na kusisitiza kuwa jukumu la kulinda mradi huo si la Serikali pekee, bali ni la kila Mtanzania, kutokana na umuhimu wake katika maendeleo ya Taifa. Mradi huu ni wetu sote, Ni lazima tuulinde, tuutunze na tuhakikishe unaendelea kutoa manufaa kwa Watanzania wa leo na vizazi vijavyo,” amesema Rais Samia. Ameongeza kuwa Mradi wa JNHP ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati inayotarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya nishati nchini, hivyo akawataka wananchi kutoa ushirikiano kwa mamlaka husika katika kulinda miundombinu ya mradi huo. Kituo cha Uzalishaji wa Umeme cha Julius Nyerere chenye uwezo wa megawati 2,115 kinatarajiwa kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini na kuimarisha upatikanaji wa nishati kwa matumizi ya majumbani, viwandani na katika shughuli mbalimbali za kiuchumi. Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratus Ndejembi amebainisha kuwa mradi huo una umuhimu mkubwa kwa maendeleo ya Taifa. Aidha, uzinduzi wa kituo hicho unafungua sura mpya katika safari ya Tanzania ya kuimarisha usalama wa nishati, huku Serikali ikiendelea kusisitiza umuhimu wa wananchi kuwa washiriki wakuu katika kulinda na kunufaika na miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa nchini.