JHNPP: Safari Yenye Vikwazo Vingi Iliyokamilika kwa Ushindi Mkubwa
Na Jacqueline Mrisho MAELEZO.
Hatimaye Tanzania imeshuhudia kutimia kwa maono ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, ya kujenga bwawa katika eneo la Stiegler’s Gorge kwenye Mto Rufiji kwa ajili ya kuzalisha umeme wa uhakika na wa kutosha kwa maendeleo ya Taifa.
Wazo hilo lililoanzishwa na Serikali ya Awamu ya Kwanza chini ya uongozi wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1976 liliendelea kuenziwa na viongozi waliomfuata, wakiwemo Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi, Hayati Benjamin William Mkapa na Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.
Licha ya kukabiliwa na changamoto na upinzani mbalimbali ndani na nje ya nchi, Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ilichukua hatua ya kutafuta fedha, kutatua changamoto na kuanza utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa kimkakati.
Leo, Bwawa la Mwalimu Nyerere limekuwa sehemu muhimu ya jitihada za Tanzania kuhakikisha Taifa linakuwa na umeme wa kutosha, wa uhakika na wenye uwezo wa kuchochea shughuli za kiuchumi na kijamii.

Mradi huo una uwezo wa kuzalisha Megawati 2,115, hatua inayoongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa Taifa kuzalisha umeme na kusaidia kuondoa changamoto ya upungufu na mgao wa umeme uliokuwa ukiathiri uzalishaji viwandani, huduma za jamii, biashara na matumizi ya majumbani.
Umeme huo umefungua nafasi kubwa kwa uwekezaji, viwanda, biashara, utalii, uzalishaji na ajira, huku ukitoa fursa ya kuongeza kipato cha wananchi na kuchangia ukuaji wa Pato la Taifa.
Akizindua mradi huo Agosti 22, 2026, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alisema kukamilika kwa mradi huo ni fundisho kwamba mafanikio ya miradi ya kimkakati yanahitaji uthubutu, uthabiti na ufuatiliaji wa karibu.
Tunapofanya maamuzi yenye maslahi kwa Taifa, hatupaswi kukata tamaa kwa sababu njia ya kufanikisha ni ngumu bali tunapaswa kuwa na uthubutu na uthabiti wa kuyasimamia maono na maamuzi yetu ili kufikia malengo tuliyojiwekea na manufaa tunayoyatarajia, alisema Rais Samia.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhe. Felischem Mramba, amesema mahitaji ya umeme nchini yanaongezeka kwa kati ya asilimia 10 hadi 15 kwa mwaka, hali inayoashiria pia ukuaji wa shughuli za kiuchumi.
Amesema Bwawa la Mwalimu Nyerere limekuwa msingi muhimu wa kuondoa mgao wa umeme na kuwezesha Tanzania kuendelea na uwekezaji katika uchumi wa viwanda, kuvutia wawekezaji, kuimarisha utalii na kukuza shughuli nyingine za uzalishaji.
Bwawa hili limetutoa kwenye mgawanyo wa umeme kama nchi, na linatuhakikishia sasa kwamba tunaweza kuendelea kuwekeza kwenye uchumi wa viwanda, tunaweza kualika wawekezaji kutoka nje wakaja kuwekeza kwenye uchumi wetu, tunaweza kuboresha utalii na mambo mengine mbalimbali ambayo ndiyo hasa yanayokuza uchumi wetu, amesema.
Kukamilika kwa bwawa hilo ni hatua moja katika kuhakikisha umeme unaowafikia wananchi wote. Serikali inaendelea kuimarisha Gridi ya Taifa, ikiwemo kukamilisha njia ya umeme ya kilovoti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma yenye urefu wa kilomita 345, pamoja na upanuzi wa kituo cha kupokea na kupooza umeme cha Zuzu, Dodoma.
Kupitia kituo hicho, umeme kutoka Bwawa la Mwalimu Nyerere unasafirishwa kwenda Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Kanda ya Kati, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Magharibi na Kanda ya Kaskazini.

Jitihada hizo zimepanua wigo wa upatikanaji wa umeme, ambapo hadi sasa vijiji vyote 12,318 na takribani asilimia 62.4 ya vitongoji Tanzania Bara vimefikiwa na huduma hiyo. Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha nchi nzima inapata umeme ifikapo mwaka 2030.
Uwezo mkubwa wa uzalishaji umeifanya Tanzania kuwa na umeme wa ziada, unaoweza kutumika kwa mahitaji ya ndani na kuuzwa katika nchi jirani ili kuongeza mapato na upatikanaji wa fedha za kigeni.
Tayari Tanzania imepokea maombi kutoka nchi mbalimbali. Zambia imeonesha hitaji la kati ya Megawati 500 na 600, Rwanda inahitaji Megawati 100, huku Kenya ikikubaliana na Tanzania kuhusu uwezekano wa kufanya mabadilishano ya umeme.
Hii inaifanya Tanzania kuingia katika hatua mpya, ambapo umeme hauwi tu huduma muhimu kwa maendeleo ya ndani, bali pia bidhaa yenye uwezo wa kuzalisha mapato na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na nchi jirani.
Pamoja na Bwawa la Mwalimu Nyerere, Serikali inaendelea kuwekeza katika vyanzo vingine vya nishati, ikiwemo jua, upepo na nishati ya jotoardhi (thermal), ili kuongeza uwezo wa Taifa kuzalisha umeme kulingana na kasi ya ukuaji wa uchumi.
Hatua hizi zinaifanya Tanzania kujenga msingi wa nishati unaoweza kuhimili mahitaji ya sasa na ya baadaye, huku ukifungua milango zaidi kwa viwanda, uwekezaji, biashara na ajira. Kukamilika kwa Bwawa la Mwalimu Nyerere si mwisho wa safari, bali ni mwanzo wa hatua mpya ya Tanzania yenye nishati ya kutosha, uchumi unaokua na fursa zinazoongezeka kwa wananchi.